Majaliwa awaonya wanaotorosha dhahabu

November 29, 2021 2:59 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo Novemba 29, 2021 ametembelea kiwanda cha kuchenjua madini cha ‘Giant Elution’ kilichopo Chunya Mkoani Mbeya. Picha| Ofisi ya Waziri Mkuu.


  • Awataka kutumia masoko ya ndani kujipatia faida.
  • Asema masoko yasiyo rasmi yanaikosesha Serikali mapato.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka wafanyabiashara katika sekta ya madini kuuza madini yao katika masoko ya madini yaliyoanzishwa Tanzania badala ya kuuza madini hayo katika masoko yasiyo rasmi hasa nje ya nchi.

Majaliwa amesema hakuna sababu ya kutorosha madini kwani kwa kufanya hivyo nchi inapoteza mapato ambayo yanaiwezesha Serikali kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kutoa huduma muhimu za jamii ikiwemo sekta za afya, elimu na maji.

“Haipendezi sana kwa baadhi ya watu kuendelea na tabia ya kukimbiza dhahabu yetu kwenda kuuza kwenye ‘black market’ (masoko yasiyo rasmi), Serikali yetu imeweka mazingira mazuri ya uuzaji wa madini, kila wilaya inayozalisha madini tumeweka masoko tena yanatoa bei nzuri,” amesema Majaliwa.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Novemba 29, 2021 alipotembelea kiwanda cha kuchenjua madini cha ‘Giant Elution’ kilichopo Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya.

Aidha, Majaliwa ametoa wito kwa watanzania kuendelea kuwekeza katika sekta ya madini kwani Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji imeweka mazingira bora kwa wawekezaji wazawa.

“Maafisa wa madini hakikisheni mnawatembelea wachimbaji wadogo, muwaelimishe pamoja na kuwawezesha kupata fursa katika taasisi za kifedha ili waweze kupata mikopo itakayo wawezesha kununua vifaa vya kisasa na kuongeza tija katika uchimbaji wao,” amesema.

Waziri Mkuu amesema amefurahishwa na taarifa ya Wilaya ya Chunya kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato katika sekta ya madini na kuwapongeza viongozi wa wilaya na mkoa kwa kuwa na usimamizi mzuri pamoja na ukusanyaji wa mapato.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mheshimiwa Juma Homera, amesema mkoa wa madini wa Chunya walikuwa wanakusanya kilo 20 za dhahabu kwa mwezi lakini baada ya masoko kuanza wanakusanya kilo 250 hadi 300 ambayo hadi sasa wamekusanya tani 6.4 yenye thamani ya Sh719.6 bilioni.

“Serikali imepata zaidi ya Sh43.2 bilioni kama sehemu ya mrahaba na Sh7.2 bilioni kama ada ya ukaguzi ambapo jumla Serikali imepata Sh50.3 bilioni,” amesema Homera.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW