Majaliwa atoa mwelekeo mpya waliopata namba ya utambulisho wa Taifa

January 30, 2020 7:40 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Aagiza wote wenye namba hizo waruhusiwe kupata huduma zote zinazohitaji kitambusho cha Taifa.
  • Mitambo, watumishi waongezwa makao makuu ya Nida, halmashauri kuharakisha zoezi la utoaji vitambulisho hivyo.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameagiza wananchi wenye namba ya utambulisho wa Taifa (NIN) waruhusiwe kupata huduma zote zinazohitaji kitambulisho cha Taifa wakati Serikali ikishughulikia upatikanaji wa haraka wa vitambulisho vyao kutoka Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida). 

Namba ya NIN imeanza inatumika katika usajili wa laini za simu kwa alama za vidole kwa wale ambao wamepata tayari. 

“Tunachokifanya sasa ili Watanzania waweze kupata huduma yoyote ile inayohitaji kitambulisho cha Nida, Serikali imeridhia kila yeyote anayetaka kitambulisho cha Nida na kama mwananchi hatakuwa hajapata kitambulisho cha Nida basi atumie namba ili kuweza kuhalalisha kupata huduma yoyote ile inayohitaji kitambulisho huku akiwa anasubiri kitambulisho,” amesema Majaliwa leo (Januari 30, 2020) bungeni jijini Dodoma.

Majaliwa alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Manyovu, Albert Obama katika kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu aliyetaka kujua kauli ya Serikali katika kuongeza kasi ya upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa hasa  maeneo ya vijijini. 


Soma zaidi: 


Waziri Mkuu amekiri kuwa ni kweli kuwa Watanzania wengi hasa wa vijini hawajafikiwa na huduma za utoaji vitambulisho hivyo, lakini Serikali inafanya kila liwezekanalo kuwafikia kwa wakati. 

Aidha, amesema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu kuhakikisha Nida wanaongeza kasi ya kutengenezwa na kugawa vitambulisho vya Taifa kwa watu ambao tayari wana namba ya utambulisho kokote waliko.  

“Hiyo ndiyo njia tumerahisisha ili kuwafikia Watanzania wote mpaka vijijini na kuhakikisha kwamba uchapishaji wa vitambulisho makao makuu (ya Nida) kule Kibaha iende kwa haraka na vitambulisho vipelekwe mpaka vijijini kwa haraka ili kila Mtanzania aweze kupata vitambulisho,” amesisitiza Majaliwa. 

Katika kufanikisha zoezi hilo la uchapaji na ugawaji wa vitambulisho, amesema wameongeza mitambo ya kufanyia kazi na idadi ya watumishi wa Nida katika ngazi ya halmashauri  na makao makuu ili kuwezesha kufika katika vijiji na vitongoji na kufanya kazi hiyo.

Kwa mujibu wa Nida, hadi kufikia Januari 2, 2020, watu milioni 7.6 walikuwa wamepata namba za utambulisho wa Taifa nchi nzima wakisubiri kupata vitambulisho vyao. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW