Maboresho sekta ya sheria yaokoa Sh9.01 bilioni za kuwalipa mawakili
Hata hivyo, amesema Serikali itaendelea kutumia mawakili binafsi kwa kibali cha Mwanasheria Mkuu wa Serikali pale itakapothibitika kuwa ni lazima kufanya hivyo. Picha|Mtandao.
- Fedha hizo zimeokolewa mwaka 2018/2019 baada ya kuanzishwa kwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali.
- Awali Serikali ilikuwa inatumia kampuni binafsi za uwakili kuendesha mashauri.
- Imesema katika baadhi ya mashauri itaendelea kuwatumia mawakili binafsi.
Dar es Salaam. Kutokana na mabadiliko makubwa yaliyofanyika katika sekta ya sheria nchini, Serikali imeeleza kuwa imefanikiwa kuokoa takriban Sh9.01 bilioni ambazo zingetumika kulipa makampuni binafsi ya uwakili kuendesha mashauri ya taasisi za Serikali.
Baadhi ya maboresho hayo ni kuanzishwa kwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambayo imepewa mamlaka ya kusimamia, kuendesha na kuratibu mashauri yote ya madai kwa niaba ya Serikali.
Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Dk Augustine Mahiga ametoa maelezo hayo Bungeni leo (Juni 18, 2019) wakati akijibu swali la Mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea ambae alitaka kujua kiasi cha fedha ambacho serikali imeokoa tangu maboresho kwenye sekta hiyo yaanze kutekelezwa.
Dk Mahiga amesema katika mwaka wa fedha wa 2018/2019 pekee Serikali imeweza kuokoa takriban Sh9.01 bilioni ambazo kama siyo maboresho kwenye sekta hiyo zingetumika kulipa makampuni binafsi ya uwakili.
Soma zaidi:
- Serikali yapendekeza mabadiliko makali Sheria ya Takwimu
- Balozi Mahiga azungumzia sheria za uwekezaji Tanzania
Hata hivyo, amesema Serikali itaendelea kutumia mawakili binafsi kwa kibali cha Mwanasheria Mkuu wa Serikali pale itakapothibitika kuwa ni lazima kufanya hivyo.
Ametoa mfano wa vigezo vinavyotumika kutumia mawakili binafsi ni pamoja na shauri kufunguliwa katika mahakama ambazo siyo za kimataifa na sheria za nchi husika haziruhusu uwakilishi wa Mwanasheria kutoka nje ya nchi hiyo.
Katika kuhakikisha maslahi ya Taifa yanalindwa, Waziri huyo ameliambia Bunge kuwa uendeshaji wa mashauri hayo utaendelea kuishirikisha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwenye kila hatua ya mwenendo wake tofauti na hapo awali.
Kuhusu baadhi ya mashirika ya umma kuendelea kutumia mawakili binafsi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Profesa Adelardus Kilangi amesema mashirika hayo ni yale ambayo mashauri yake yalianza kabla ya maboresho hayo hayajaanza kutekelezwa.