LHRC: Ubaguzi bado ni changamoto sekta ya biashara
Wanawake wakiwa sokoni katika kujitafutia riziki. Picha| Burudani Mwanzo.
- Ripoti mpya ya LHRC inaonyesha kuwa ubaguzi wa kijinsia umekithiri katika sekta ya biashara nchini.
- Ubaguzi katika ajira kwa watu wenye ulemavu bado ni kizungumkuti.
- Wadau walia na uwajibikaji kwa serikali na watu binafsi katika kukomesha ubaguzi wa aina yoyote.
Dar es Salaam. Kuwepo kwa ubaguzi katika sehemu mbalimbali za kazi na maeneo ya biashara sio kitu kigeni katika masikio ya wengi hasa katika harakati za kusaka fursa mbalimbali katika jamii.
Ubaguzi umekuwa katika sura mbalimbali ukihusisha masuala ya ukabila, jinsia na hata maumbile kutokana na eneo husika.
Ripoti mpya ya Haki za Binadamu na Biashara mwaka 2017, iliyotolewa na kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) hivi karibuni inabainisha wanawake wanakabiliwa na changamoto ya kubaguliwa katika maeneo yao ya biashara na kazi licha ya kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi hasa kupitia sekta isiyo rasmi na sekta binafsi.
Wanawake hao mbali na unyanyasaji wa kijinsia ikiwemo ukatili wa kingono unaofanywa na baadhi ya maafisa kwenye sekta ya biashara, wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa mtaji, ugumu katika kupata mikopo nafuu na baadhi ya hunyimwa haki ya kumiliki mali hivyo kukosa dhamana ya mikopo.
Ripoti hiyo imebaini uwepo wa ubaguzi wa kijinsia kazini na katika mchakato wa utafutaji wa ajira lakini wafanyakazi wengi walioshiriki kwenye utafiti huo walisema hakuna ukatili wa kijinsia mahala pao kwa kazi. Majibu hayo, kwa mujibu wa watafiti wa LHRC, yalitokana na uelewa mdogo wa masuala ya ukatili wa kijinsia.

Chanzo: Ripoti ya Haki za Binadamu na Biashara mwaka 2017 ya LHRC.
Ripoti hiyo inaeleza zaidi kuwa matukio ya ukatili wa mwili yalitajwa zaidi makazini na wafanyakazi ambao wapo kwenye menejimenti za kampuni. Ukatili huo unaendana na kuendelea kwa vitisho kwa wafanyakazi.
Felister Mahuya wa LHRC anasema suala la ubaguzi katika sehemu zozote za ajira lifanyiwe kazi na kupingwa na kwamba ni jukumu la wananchi na wadau wote nchini kuongeza uelewa juu ya kuondoa tatizo hilo.
“Ni jukumu la kila mmoja kuzingatia sheria katika maeneo ya kazi na biashara na ajitafakari kwa nafasi yake nini anafanya,” anasema Felister.
Ili kutokomeza ukatili wa kijinsia katika eneo la biashara na kazini, wadau wanasema kuwa wanaendelea kutoa elimu kuhusu haki za wafanyakazi na wafanyabiashara wa makundi yote kwa kufanya kazi bila ubaguzi wowote ule.
“Tunatoa semina kwa waajiri na wafanyakazi wa sekta mbalimbali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha hawabagui na kuwanyanyasa walemavu katika maeneo ya kazi, na pia tunatoa ushauri kwa Serikali kufuata Sera ya Taifa ya Ulemavu ya mwaka 2004,” anasema Ummy Nderiananga, Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu Tanzania (Shivyawata).
Latest
