Kicheko kwa wakulima: Serikali kusamehe kodi bima ya kilimo

June 12, 2020 9:29 am · TULINAGWE ALSON
Share
Tweet
Copy Link
  • Imependekeza kusamehe kodi ya ongezeko la thamani kwenye bima za kilimo cha mazao
  • Lengo ni kuongeza kasi ya wakulima kukata bima za kilimo ili kujilinda na majanga ya athari. 
  • Itawasaidia kupata dhamana ya mikopo katika taasisi za fedha.  

Dar es Salaam. Huenda wakulima wa Tanzania watapata tija kwenye shughuli za kilimo baada ya Serikali kutangaza kuwa itapunguza gharama za upatikanaji wa bima ya mazao nchini. 

Kwa muda mrefu wakulima wamekuwa wakijihusisha na kilimo lakini changamoto inayowakabili ni uhakika na usalama wa mavuno wanayoyapata kila mwaka, jambo ambalo limekuwa likiwakosesha mapato lukuki. 

Serikali imesema inakusudia kufanya marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani sura ya 148 yatakayosamehe kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwenye bima ya kilimo cha mazao ili kupunguza gharama na kutoa unafuu katika bima za kilimo.

Waziri wa fedha na mipango Dk Philip Mpango amesema lengo la hatua hii ni kupunguza gharama na kutoa unafuu katika bima za kilimo ili kuwawezesha wakulima kuziwekea bima shughuli za kilimo na kuvutia wananchi kutumia huduma za bima kwa ajili ya kujikinga na majanga mbalimbali yanayoathiri shughuli zao za kilimo ikiwemo ukame na mafuriko.


Zinazohusiana:


Bima hiyo ilizinduliwa na Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga mwaka 2019 na inasimamiwa na Shirika la Bima la Taifa (NIC).

Bima ya mazao inamsadia mkulima kujikinga na athari za majanga ya asili na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kupata dhamana ya mikopo katika taasisi za fedha. 

Sambamba na hilo, Serikali itafanya marekebisho ya kuwawezesha wauzaji wa bidhaa ghafi nje ya nchi kuendelea kujirudishia Kodi ya VAT iliyolipwa kwenye gharama za huduma au bidhaa katika shughuli hizo ili bidhaa hizo ziweze kushindana katika masoko ya nje. 

“Hatua hii pia inalenga kuendana na msingi wa utozaji VAT kwa kuzingatia mahali bidhaa inapotumika (destination principle). Hatua zote za kodi ya ongezeko la thamani kwa ujumla wake zinatarajiwa kupunguza mapato ya Serikali kwa kiasi cha Sh46 milioni,” amesema Dk Mpango.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW