Kamwelwe: Utatuzi wa changamoto za hali ya hewa unahitaji nguvu ya pamoja
- Amesema Serikali inaendelea kuwekeza katika huduma za hali ya hewa ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya uangazi na kununua vifaa vya kisasa ili kutatua changamoto za hali ya hewa nchini.
Dar es Salaam. Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe amesema Serikali inaendelea kuwekeza katika huduma za hali ya hewa ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya uangazi na kununua vifaa vya kisasa ili kutatua changamoto za hali ya hewa nchini.
Kamwelwe aliyekuwa akizungumza leo (Machi 23, 2019) katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani “World Meteorological Day (WMD)” kwa mwaka 2019 jijini Dar es Salaam ambapo amesema mpaka sasa Serikali tayari imenunua rada mbili za hali ya hewa ambazo zimewekwa Dar es Salaam na Mwanza. Rada nyingine tatu zinatarajiwa kuwekwa Mtwara, Mbeya na Kigoma na ziko katika hatua za ununuzi.
Amsema katika kuimarisha zaidi huduma za hali ya hewa nchini, Serikali itaendelea kununua vifaa vingine kulingana na upatikanaji wa bajeti, na hivyo amewataka wadau mbalimbali kushirikiana katika kutatua changamoto ikiwemo gharama kubwa za vifaa, kuendana na mabadiliko ya kukua kwa teknolojia katika tasnia ya hali ya hewa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi (Climate Change).
“Utatuzi wa changamoto hizi unahitaji jitihada za pamoja za wadau mbalimbali,” amesema Kamwelwe.
Akizungumzia Siku ya Hali ya Hewa Duniani, amesema ni muhimu kwa sababu inatupa nafasi ya kutafakari mchango wa Tanzania, kama mwanachama wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) katika utoaji wa huduma za hali ya hewa hapa Tanzania na ulimwenguni kote.
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ndiyo taasisi iliyopewa jukumu la kusimamia na kutoa huduma za hali ya hewa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Ninatoa wito kwa wadau wote wa hali ya hewa kutoka sekta zote za kiuchumi na kijamii na wananchi kwa ujumla kuendelea kufuatilia na kutumia huduma za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa ajili ya kupanga na kufanya maamuzi katika shughuli za kiuchumi na kijamii kwa ajili ya ustawi wa Taifa letu,” amesema Mhandisi Kamwelwe.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (kushoto) amewataka wada mbalimbali kuendelea kufuatilia taarifa zinazotolewa na TMA ili ziwasaidie katika shughuli mbalimbali. Picha| The Habari.
TMA inatekeleza Programu ya Kitaifa ya Huduma za Hali ya Hewa (National Framework for Climate Servives), ambayo ni mwongozo muhimu katika utoaji na utumiaji wa huduma za hali ya hewa hapa nchini ambapo katika mwaka 2019 Tanzania imekuwa miongoni mwa nchi tatu barani Afrika zilizopata cheti cha ubora wa huduma za hali ya hewa katika usafiri na usalama wa anga (ISO 9001:2015) kwa mujibu wa Shirika la Viwango Duniani (ISO).
Zinazohusiana: TMA yatumia tamasha la Urithi Festical kutoa elimu ya hali ya hewa Dar
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi amesema katika kuimarisha upatikanaji na utumiaji wa taarifa za hali ya hewa katika kupanga shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii na kufikia maendeleo endelevu jitihada mbalimbali za kuboresha huduma za hali ya hewa katika ngazi ya kidunia na kitaifa zinafanyika.
“Uelewa kuhusu hali ya klimatolojia ya eneo husika ikiwemo mwenendo wa jua na nguvu yake, pamoja na nishati ya upepo ni muhimu sana katika kutoa mwongozo na kuongeza ufanisi na tija kwa uwekezaji unaolenga kuimarisha nishati mbadala,” amesema Dk Kijazi.
Kauli mbiu ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani mwaka huu ni “Jua, Dunia, na Hali ya Hewa (The Sun, The Earth, and the Weather)”, ambayo imelenga kutoa elimu kwa jamii na kuongeza uelewa wa sayansi ya hali ya hewa, hususan maandalizi, usambazaji na matumizi ya taarifa za hali ya hewa.