Kampuni za simu zageukia biashara ya magari ya umeme

Makao makuu ya Xiaomi Ghuangzhou, China. Picha: BBC
- Kampuni ya simu ya Xiaomi kuanza kutengeneza magari ya umeme.
- Yawekeza Sh23.2 trilioni katika biashara hiyo.
- Ushindani wachangia kampuni za simu kutafuta vyanzo vipya vya mapato.
Dar es Salaam. Ushindani katika sekta ya mawasiliano duniani unaendelea kushika kasi huku baadhi ya kampuni za simu zikianza kugeukia biashara ya utengenezaji wa magari yanayotumia nishati ya umeme, ikiwa ni njia ya kutanua wigo wa mapato.
Kampuni ya vifaa vya kielektroniki ya Xiaomi ya nchini China imetangaza mpango wake wa kufanya biashara ya utengenezaji magari ya umeme baada ya kuinunua kampuni inayochipukia (startup) ya Deepmotion kwa Dola za Marekani milioni 77.37 (Sh179.5 bilioni).
Kampuni hiyo imeeleza kuwa inataka kutanua wigo wa shughuli zake kutoka kutengeneza simu na kujihusisha na utengenezaji wa magari ya umeme ambayo yanatajwa kuwa rafiki wa mazingira.
Machi mwaka, Xiaomi ilitangaza kuwekeza Dola za Marekani bilioni 10 sawa na Sh23.2 trilioni katika biashara hiyo kwa miaka 10 ijayo.
Ununuzi wa kampuni hiyo wa startup ya Deepmotion, huenda akasaidia katika usimamizi wa huduma za uendeshaji wa biashara hiyo na kupata wataalamu wa kutengeneza magari ya umeme katika kizazi kijacho.
Hata hivyo, Xiaomi itakuwa na kibarua kigumu cha kushindana na makampuni makubwa ya magari ya umeme duniani ikiwemo Tesla, Xpeng na Nio ambayo yamewekeza mtaji wa kutosha katika biashara hiyo.
Kampuni hiyo ilitangaza kuichukua Deepmotion baada ya kuripoti kuongezeka kwa mapato yake kwa asilimia 64 katika robo ya pili ya mwaka 2021, kiwango ambacho ni kikubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
Utengenezaji wa simu janja unachangia asilimia 67.3 ya mapato ya kampuni hiyo huku akitazamia kuwa magari ya umeme yanaweza kuwa chanjo kipya na kizuri cha mapato.
Latest
