Huawei, taasisi za fedha kujadili namna ya kuishinda Corona
- Ni kupitia kongamano la mtandaoni litakalofanyika Mei 29, 2020.
- Litajadili jinsi benki zinaweza kujinasua na makali ya korona kwa kuangazia teknolojia ya simu za mkononi.
Dar es Salaam. Kampuni ya teknolojia ya Huawei imeandaa kongamano la mtandaoni kwa ajili ya kujadili jinsi maendeleo ya kidijitali yatakavyozisaidia sekta za fedha za nchi za Kusini mwa Afrika ili kuondokana na makali yanayotokana na ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19).
Kongamano hilo linalotarajiwa kufanyika Mei 29,2020 litajadili jinsi sekta ya fedha zikiwemo benki zinavyoweza kuwekeza zaidi katika mifumo ya fedha jumuishi ikiwemo matumizi ya simu ili kuendelea kuwepo katika soko la ushindani.
Taarifa iliyotolewa na Huawei imeeleza kuwa kwa sasa watu wengi haendi benki kwa kuogopa maambukizi ya COVID-19 kutokana na mikusanyiko ya watu.
“Janga hilo halitishii watu pekee bali hata uchumi wa dunia. Haya mabadiliko yanatokea wakati sekta za kibenki zinahama kutoka hatua moja hadi nyingine,” amesema Rais wa kampuni ya Huawei wa ukanda wa Kusini mwa Afrika, Chen Lei.
Amesema kuna kila sababu kwa wadau wa fedha kuja pamoja na kuangazia njia mbadala za teknolojia zitakazosaidia watu kuendelea huduma za benki kwa kutumia simu za mkononi wakiwa mahali popote bila vikwazo.
Hata hivyo, benki nyingi duniani zinatumia mifumo ya kidijitali ikiwemo simu benki lakini huduma zinatakiwa zirahisishwe na watu wengi wahamasike kutumia mifumo hiyo.
Zinazohusiana
- Benki za Tanzania zaanza kuondoa tozo za miamala ya simu
- Watumiaji wa huduma za simu benki wazidi kupaa Tanzania, wafikia milioni 23
- Neema ya BoT: Ufahamu mkoba wa ahueni wa kukabiliana na Corona Tanzania
Naye mwandishi wa kitabu cha “Bank 4.0” ambaye ni mmoja wa wasilishaji wa siku hiyo, Brett King anatarajiwa kuongelea jinsi simu zitakavyo zikomboa benki kutoka kwenye makali ya Covid-19.
Wawasilishaji wengine ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya KCB Kenya na Mwenyekiti wa Chama cha Mabenki (Bankers Association) cha Kenya, Joshua Oigara, Mkuu wa teknolojia (finetech) wa Benki ya KCB Kenya, Alex Wekunda na Mkuu wa Uchambuzi wa Takwimu na usimamizi wa biashara wa Benki ya FNB Afrika Kusini, Lucille De Kock.
Kujiunga na kongamano hilo litakalochukua takriban masaa mawili, unahitaji kujisajili kwa njia ya mtandao na kisha kufuatilia ratiba ya kongamano hilo kupitia tovuti ya Huawei.
Aidha, kongamano hilo litakuwa na msaada mkubwa kwa wadau wa sekta za kibenki kote ulimwenguni kwa sababu litawapa mtazamo mpya wa kuendesha shughuli zao ili kujipatia faida.
Latest