Hakuna agizo la lazima kwa watumishi wa umma kuwa na laini za TTCL: Dk Abbas
Mkurugenzi wa Idara ya Habari-Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dk Hassan Abbasi akifafanua jambo kwa Wanahabari ( hawapo pichani), kuhusu utekelezaji wa Serikali kwenye sekta mbalimbali, katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika Jijini Dar es Salaam, leo Alhamisi 30. Mei. 2019.
- Amesema agizo hilo linawahusu viongozi wa Serikali wanaohudumiwa na stahili za simu.
- Amesema hakuna agizo la ulazima kwa watumishi wengine kuwa na laini hizo.
Dar es Salaam. Msemaji Mkuu wa Serikali, Dk Hassan Abbas amesema madai kuwa Serikali imeagiza watumishi wote wa umma wawe na laini za mtandao wa Shirika la Mawasiliano ya Simu Tanzania (TTCL) ni ya uzushi bali agizo hilo linawahusu viongozi wanaohudumiwa na stahili za simu serikalini.
Ufafanuzi huo wa Serikali unakuja baada ya kusambaa katika mitandao ya kijamii kwa barua zinazodaiwa zimetoka katika baadhi ya halmashauri zikiwaelekeza watumishi wote katika maeneo yao kuwa na laini za TTCL.
Akitolea ufafanuzi suala hilo, Dk Abbas aliyekuwa akizungumza na Wanahabari leo (Mei 30, 2019) Jijini Dar es Salaam, amesema kuwa hakuna agizo la lazima kwa watumishi wa umma kuwa na laini za TTCL.
“Suala kwamba Serikali imeagiza Watumishi wa Umma kuwa na laini ya TTCL si sahihi, Rais John Magufuli alikuwa wazi kuwa viongozi wanaohudumiwa stahili ya simu watapewa vocha za TTCL lakini hakuna agizo la ulazima kwa watumishi wengine,” amesema Dk Abbas.
Amesema agizo la Rais Magufuli la kutumia laini za mtandao huo linawahusu viongozi wanaohudumiwa na stahili ya simu, hao ndiyo watapewa vocha za TTCL ili kufanikisha mawasiliano ya kiofisi.
#TUNATEKELEZA2019 Suala kwamba Serikali imeagiza Watumishi wa Umma kuwa na laini ya TTCL si sahihi, Rais @MagufuliJP alikuwa wazi kuwa viongozi wanaohudumiwa stahili ya simu watapewa vocha za TTCL lakini hakuna agizo la ulazima kwa watumishi wengine – Dkt. Abbasi#TanzaniaUpdate
— Msemaji Mkuu wa Serikali (@TZMsemajiMkuu) May 30, 2019
Mei 21, 2019, wakati akipokea gawio la Serikali la Sh2.1 bilioni kutoka kwa TTCL, Rais John Magufuli aliwataka viongozi na taasisi za Serikali ambazo bado hazijaanza kutumia laini za mtandao wa simu wa TTCL kwa ajili ya mawasiliano waanze mara moja ili kuliimarisha shirika hilo na kumuenzi baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
“Tusipowaimarisha hawa TTCL hawatafika popote, hiki ni chombo chetu, sijasema msiwe na laini zingine lakini kwani kuna ubaya gani Serikalini wakasema kuna watu wanalipiwa kwa simu, ukitaka kulipiwa simu ni TTCL ukitaka ya kujilipia nenda mitandao mingine ni hela yako,” alinukuliwa Rais Magufuli wakati akipokea gawio hilo.