Gazeti la Mwananchi mtandaoni lafungiwa miezi sita, lapigwa faini Sh5 milioni
- Ni baada ya kubainika kuchapisha na kutangaza habari yenye kupotosha na kuleta mkanganyiko kwenye jamii.
- Limesitishiwa leseni ya utoaji wa huduma za maudhui mtandaoni kwa miezi sita na kutakiwa kulipa faini ya Sh5 milioni.
Dar es Salaam. Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) imesitisha leseni ya utoaji wa huduma za maudhui mtandaoni ya gazeti la Mwananchi kwa miezi sita na kutakiwa kulipa faini ya Sh5 milioni baada ya kubainika kuchapisha na kutangaza habari yenye kupotosha na kuleta mkanganyiko kwenye jamii siku nne zilizopita.
Kamati hiyo katika tangazo lake kwa umma imeeleza kuwa kwa kuchapishwa na kutangazwa kwa habari hiyo Aprili 13, 2020 ni kinyume na Kanuni Na. 5 (1) (a) na 12 (I) za Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta za mwaka 2018.
Hata hivyo, kamati hiyo haijaweka bayana habari husika ambayo ilichapishwa katika akaunti za mitandao ya kijamii ya gazeti hilo na kufanya ichukuliwe hatua.
Taarifa hiyo, iliyochapishwa kwenye magazeti mbalimbali likiwemo Mwananchi leo, imeeleza leo kuwa Aprili 15, viongozi wa Mwananchi ambalo hutoa habari zake kwa Kiswahili waliitwa mbele ya kamati ili kutoa utetezi kwanini wasichukuliwe kwa kukiuka kanuni hizo za mawasiliano.

Sehemu ya tangazo la TCRA kwa gazeti la Mwananchi kuhusu kusitishiwa leseni yake ya kutoa maudhui mtandaoni kwa miezi sita.
Kamati hiyo imesema baada ya kusikiliza na kutafakari utetezi uliotolewa, ilijiridhisha kuwa gazeti hilo kupitia mitandao yake ya kijamii lilikiuka kanuni za mawasiliano na imetoa adhabu mbili ikiwemo kusitishia leseni ya kutoa huduma ya maudhui mtandaoni kwa miezi sita.
Pia wametakiwa kulipa faini ya Sh5 milioni kwa TCRA.
“Kamati imefikia uamuzi huu ili kuwapa Mwananchi Newspaper kujitambua, kujitafakari na kujipanga vizuri zaidi ili waweze kuendesha kituo chao kwa kuzingatia matakwa ya sheria, kanuni na taaluma ya habari na utangazaji,” inasomeseka sehemu ya taarifa hiyo.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- TCRA yakusudia kusimamisha leseni za DSTV na Zuku.
- CCM yazidi kuongeza umiliki wa vyombo vya habari Tanzania
Hata hivyo, akaunti za mitandao ya kijamii za gazeti hilo hazijaweka habari yoyote leo huku tovuti yake ikiwa haipatikani.
“Tovuti yetu imefungwa kwa muda, hata hivyo turajea hivi karibu na habari za uhakika kutoka Tanzania, Afrika Mashariki na duniani kote. Samahani kwa usumbufu uliojitokeza na tutakuona hivi karibuni,” inasomeka sehemu ya ujumbe kila unapotafuta tofuti ya mwananchi.
Hivi ndivyo unavyosomeka ujumbe kila unapotafuta tovuti ya gazeti la Mwananchi mtandaoni.
Latest
