Fursa kilimo cha parachichi zaendelea kufunguka Tanzania

June 27, 2020 10:03 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Serikali yawataka wakulima kuongeza uzalishaji wa zao hilo kwa ubora unaokidhi viwango vya kimataifa.
  • Mauzo nje ya nchi yaongezeka takriban mara tatu ndani ya miaka mitatu.
  • Mauzo yenye thamani ya zaidi ya Sh19.6 bilioni.

Dar es Salaam. Wakulima nchini Tanzania wametakiwa kuchangamkia fursa za kilimo cha parachichi ili kunufaika na soko lake ikizingatiwa kuwa mauzo ya zao hilo nje ya nchi yameongezeka takriban mara tatu ndani ya miaka mitatu.

Takwimu zilizotolewa na Wizara ya Kilimo mwaka huu zinaeleza kuwa kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa parachichi mauzo yake nje ya nchi yameongezeka kutoka tani 3,279 mwaka 2015 hadi tani 9,000 mwaka 2018. Hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 63.5 ndani ya miaka mitatu. 

Mauzo hayo yenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 8.5 (Sh19.6 bilioni) yamefanyika katika soko la Ulaya katika nchi za Ufaransa, Uholanzi na Uingereza.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki amesema zao hilo ni malighafi ya utengenezaji wa bidhaa mbalimbali hivyo linahitajika kwa wingi sokoni. 

“Tumieni fursa ya zao hili kwa kuzingatia lina matumizi mengi ikiwemo mafuta ya kula, dawa pamoja na kuchanganya katika vipodozi mbalimbali vinavyotumika kwa matumizi ya binadamu,” amesema Kairuki alipotembelea miradi ya kilimo mkoani Njombe Juni 24, 2020.


Zinahusiana:


Amesema awali zao hilo lilikuwa na mauzo hafifu kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya hali hewa lakini sasa mauzo yameongezeka kutokana na kuimarika kwa soko.

Amesema zao la parachichi limeendelea kuwa na tija nchini, hivyo wakulima wanapaswa kuchangamkia fursa hiyo ili kujikwamua kiuchumi.

“Parachichi ni zao linalokua kwa kasi kwa kuangalia hapo nyuma uzalishaji ulikuwa takribani tani 20,000 pekee ingawa kwa kipindi cha miaka minne tangu Serikali ya awamu ya tano iingie madarakani kumekuwa na ongezeko kubwa la zaidi ya mara tisa na nusu kufikia tani 190,000 kwa mwaka,” amesema Kairuki. 

Zao la parachichi ni miongoni mwa mazao ya bustani ambalo hutegemewa kiuchumi na wakulima wa mikoa ya Iringa, Mbeya, Njombe, Katavi, Rukwa, Ruvuma, Kilimanjaro na Morogoro.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW