Boda boda Arusha wabuni mfumo wa kudhibiti uhalifu

August 10, 2024 3:48 pm · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Kila bodaboda kupewa namba na mavazi maalum ya utambulisho.
  • Usajili huo utawewezesha kupata mikopo kwa urahisi kutoka Serikalini na Sekta binafsi.

Arusha. Waendesha pikipiki maarufu kama boda boda mkoani Arusha wameanzisha mchakato wa urasimishaji wa kazi hiyo kwa njia ya namba za usajili wa pikipiki ili kupunguza vitendo vya uhalifu na kuongeza maslahi ya kiuchumi

Kwa miaka kadhaa madereva hao wamekuwa wakihusishwa na vitendo vya uhalifu kama wizi na uporaji ambapo Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Arusha Mjini, Hassan Mndeme vitendo hivyo vimekuwa vikichafua sifa ya  mkoa huo

“Vitendo vya uhalifu mkoa wa Arusha vinachafua hadhi ya mkoa huu tunaamini kila boda boda akijisajili itakuwa rahisi kutambua nani ni muhalifu na nani hausiki,” amesema Mndeme alipokuwa akizindua ofisi ya boda boda kata ya Sokoni jijini Arusha leo Agosti 10, 2024.

Akizungumza na Nukta Habari Hakimu Msemo Katibu wa Boda Boda wilaya ya Arusha amesema kuwa mfumo huo utaweka utaratibu maalum wa kuwatambua waendesha boda boda kutoka vituo vyao vya kazi, kata na wilaya hivyo kurahisisha kudhibiti wahalifu.

“Cha msingi ni kukazana kushirikiana na Serikali kuhakikisha boda zote mkoa wa Arusha ziingie kwenye mfumo zikishaingia hatutasumbuana na uhalifu wa boda boda,” amesema Hakimu.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo mpaka Sasa waendesha boda boda 6,500 kati ya 12,000 waliopo mkoani Arusha wamesajiliwa na wanasubiri utaratibu wa namba za utambuzi pamoja na kupewa mavazi maalum(reflector) utakaofanywa na Serikali ya mkoa huo kwa kushirikiana na wadau wa sekta binafsi.

Mchakato wa usajili kwa waendesha boda boda utaanzia katika ofisi za boda boda za kata na taarifa zao kuhamishiwa wilayani na mkoani.

Namba na ‘reflector’ feki kudhibitiwa

Hakimu amebainisha kuwa wamejipanga vyema kudhibiti wahalifu wote watakaotumia namba za usajili pamoja na reflector feki na wakibainika hatua kali dhidi yao zitachukuliwa.

“Tutajaribu kutengeneza sare ambazo zitashindwa kuibwa, pia tutakuwa na doria sisi wenyewe kugundua wenye sare feki na tutaamuru wakamatwe,” ameongeza Hakimu.

Kwa upande wa waendesha boda boda ambao hawatavaa sare hizo maalum na kuwa namba hizo za utambulisho Hakimu amesema kuwa watazuiwa kupakia abiria pamoja na kuchukuliwa hatua za kisheria.

Katika hatua nyingine usajili huo unatarajiwa kulinda haki za bodaboda kutoka kwa wamiliki wa vyombo moto huku ikiwasaidia kupata mikopo ya Serikali na sekta binafsi kwa urahisi.

“Tunajua kuwa bodaboda mnahitaji mikopo mkisajiliwa itakuwa rahisi kuipata serikalini na hata katika ofisi yenu ambayo leo mnaizindua naamini hamuwezi kushindwa kukopeshana kwa sababu mtakiwa mnajuana, amesema Mwenyekiti Mndeme.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW