Balozi Kijazi awataka wahandisi kuchangamkia fursa za miradi ya ujenzi Tanzania

September 6, 2018 11:21 am · TULINAGWE ALSON
Share
Tweet
Copy Link
  • Wahandisi waambiwa na Balozi Kijazi watafute fursa kwenye sekta ya ujenzi nchini badala ya kulalamikia ushindani.
  • ERB waeleza kuwa wataendelea kufanya kazi kwa weledi na kuchangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Dar es Salaam. Wahandisi wazawa nchini wameshauriwa kuacha tabia ya kulalamikia ushindani unaojitokeza kwenye sekta ya ujenzi badala yake wachangamkie fursa za miradi ya ujenzi kila inapojitokeza ili kuwa sehemu ya kukuza uchumi wa Taifa.

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi ametoa ushauri huo katika maadhimisho ya miaka 50 ya Bodi ya Uandisi (ERB) yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam yakilenga kutathmini mchango wa bodi hiyo katika kuimarisha na kukuza uchumi wa Tanzania ikizingatiwa kuwa miundombinu inayojengwa kama barabara, majengo yamekuwa kichocheo cha biashara na usafiri.

Balozi Kijazi amesema wahandisi ni sehemu muhimu ya kukuza uchumi wa nchi hivyo ni muhimu kuchangamkia fursa za miradi ya ujenzi zinazotolewa na Serikali na mashirika binafsi ili kuwezesha mzunguko mzuri wa fedha na kukuza kipato kwa watanzania.  

“Ndugu wahandisi ni jukumu letu kuchangamkia fursa zinazojitokeza na kuhakikisha tunazifanyia kazi ipasavyo” amesema Balozi Kijazi.

Kwa nyakati tofauti wahandisi wazawa wamekuwa wakilalamika kukosa zabuni za kujenga miundombinu wakidai kampuni kutoka nje ya nchi ndiyo zinapewa kipaumbele.  

Amesema ufanisi na utendaji mzuri katika kazi wanazopewa unaweza kuwasaidia kupata zabuni nyingi za ujenzi na kuwawezesha kuimarisha kampuni zao kushindana na wawekezaji wa kimataifa.

Wahandisi kutoka taasisi mbalimbali wakiwa katika ukumbi wa Diamond Jubilee wakati wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Bodi ya Waandisi (ERB) Jijini Dar es Salaam. Picha | Tulinagwe Malope.

Maadhimisho ya miaka 50 ya ERB yanafanyika siku tatu (Septemba 5 hadi 7, 2018) katika ukumbi Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam ambapo yanahusisha shughuli mbalimbali ikiwemo maonyesho ya kampuni na teknolojia ya ujenzi.

 Mwenyekiti wa Bodi ya ERB, Prof Ninatubu Lema amesema wataendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza uchumi wa Taifa kwa kuzingatia maadili ya kazi zao.  

“Kiasi kikubwa Wahandisi wanapaswa kuchangia na kuimarisha sekta ya ujenzi nchini kwa kukuza na kuwezesha miradi mbalimbali na kuwezesha vijana walioko shule,” amesema Prof Lema.

Bodi ya ERB ilianzishwa mwaka 1968 baada ya Azimio la Arusha mwaka 1967 ambapo mpaka sasa ina wanachama 22,226 wanaotoka katika sekta mbalimbali za ujenzi nchini.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka 50 ya ERB, wahandisi wanapaswa kufanya tathmini ya mchango wanaoutoa katika jamii na ukuaji wa uchumi.

 “Kutimiza miaka 50 ni lazima watu wajiulize maswali magumu ili kupima ni kwa namna gani uchumi wa nchi umezidi kuimarika,” amesema  Prof Lema.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW