Askofu Tutu alikuwa mnara wa amani duniani-Guterres

December 27, 2021 6:47 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Alikuwa mshindi na tuzo ya Nobel aliyesaidia kumaliza ubaguzi wa rangi nchini humo.
  • Viongozi mbalimbali waomboleza kifo chake akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan.
  • Askofu Desmond Tutu wa Afrika Kusini amefariki jana akiwa na miaka 90.

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) António Guterres ameelezea masikitiko yake kufuatia kifo cha Askofu Desmond Tutu wa Afrika Kusini akimwelezea kuwa mtu aliyepaza sauti za wasio na sauti bila uoga wowote.

Kifo cha Askofu Tutu (90) kimetangazwa Desemba 26, 2021 na Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa.

Rais Ramaphosa amesema kwamba kifo cha muhudumu huyo wa kanisa na Mshindi wa tuzo ya Nobel ambaye aliisaidia Afrika Kusini kumaliza ubaguzi wa rangi ni miongoni mwa msiba mkubwa wa kitaifa katika kizazi muhimu cha taifa hilo.

Msemaji wa UN iliyotolewa jana jijini New York nchini Marekani imemnukuu Katibu Mkuu akisema “Askofu Desmond tutu alikuwa mnara wa amani duniani na mtoa hamasa kwa vizazi tofauti duniani kote. Wakati wa kipindi kigumu cha ubaguzi wa rangi, alikuwa nguzo ya nuru ya haki, uhuru na kusaka haki bila ghasia.”

Guterres amesema azma ya Askofu Tutu ya kujenga mshikamano wa dunia kwa ajili ya Afrika Kusini huru ilitambuliwa vyema na Kamati ya utoaji wa tuzo za Nobel mbapo mwaka 1984 ilimtunuku tuzo ya amani ya Nobel.

Akiwa mwenyekiti wa Kamisheni ya ukweli na maridhiano Afrika Kusini, Askofu Tutu alitoa mchango mkubwa wa kuhakikisha kipindi cha amani na cha haki cha mpito wa kidemokrasia nchini Afrika Kusini.

Guterres amesema busara zake na uzoefu mkubwa aliokuwa nao kila wakati alivitumia kuwasilisha hoja zake kwa utu, ucheshi na moyo wa dhati.

Akizungumzia mchango wake katika ushirikiano wa kimataifa, Guterres amesema Askofu Tutu alikuwa mchechemuzi wa ushirikiano wa kimataifa na alikuwa na dhima muhimu akitolea mfano mchango wake kama mjumbe wa kipekee wa Kamati ya ushauri ya Umoja wa Mataifa katika kuzuia mauaji ya kimbari na katika ujumbe wa ngazi ya juu wa kusaka ukweli huko ukanda wa Gaza mwaka 2008.

Katika miongo ya hivi karibuni, Askofu tutu aliendelea kupigania kwa dhati kuchukuliwa kwa hatua katika masuala kadhaa kama vile umaskini, mabadiliko ya tabianchi, virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi.

“ingawa kifo cha Askofu Tutu kinaacha pengo kubwa kimataifa na katika nyoyo zetu, daima tutahamasika na mfano wake kuendeleza mapambano ya kuhakikisha dunia inakuwa pahala bora kwa kila mtu,” amesema Guatteres katika taarifa hiyo.

Rais Samia atoa salamu

Rais Samia ameungana na viongozi mbalimbali duniani kuomboleza kifo cha Tutu akimtaja kuwa alikuwa nguzo muhimu ya mapambano ya ukombozi wa Afrika.Ametoa pole kwa Rais Ramaphosa na raia wa Afrika Kusini kwa kuondokewa na mtu muhimu aliyechangia kuimarisha amani na utulivu katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika.

Kifo cha Askofu Tutu aliyewahi kuwa  Askofu Mkuu wa kanisa la Anglikana kimetokea  wiki chache baada ya Rais wa mwisho wa enzi za ubaguzi wa rangi Frederik Willem de Klerk kufariki akiwa na umri wa miaka 85.

Mwili wa Tutu unatarajiwa kupumzishwa katika nyumba yake ya milele katika jiji la Cape Town Januari Mosi, 2022. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW