Alichokisema Makamba baada ya Bashe, Simbachawene kuapishwa
- Asema hilo ndilo neno lake la mwisho.
- Amewapongeza na yuko tayari kushirikiana na mawaziri hao.
- Amemshukuru Rais kwa kumuamini na watendaji wa wizara yake kwa ushirikiano waliompa.
Dar es Salaam. Aliyekuwa Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba ametoa “neno la mwisho” baada ya kufutwa uwaziri huku akieleza kuwa yuko tayari kushirikiana na mawaziri wawili waliopishwa leo, George Simbachawene aliyechukua nafasi yake na Hussein Bashe aliyeteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Kilimo.
Mawaziri hao wameapishwa leo (Julai 22, 2019) Ikulu Jijini Dar es Salaam na Rais John Magufuli baada ya mabadiliko madogo katika Baraza la Mawaziri yaliyofanyika jana na kumtupa nje Makamba.
Katika ukurasa wa Twitter, Makamba amesema anamshukuru Rais kwa kumuamini kwa nafasi aliyotumikia tangu mwaka 2015 alipoteuliwa na watendaji wote walioshirikiana naye kutimiza majukumu ya ofisi.
Amewapongeza Bashe na Simbachawene kwa kuteuliwa na amebainisha kuwa yuko tayari kuwapa ushirikiano wowote watakaotaka kutoka kwake.
Neno la Mwisho kwenye hili:
Namshukuru Rais kwa kuniamini, Makamu wa Rais kwa kunielekeza, PM kwa kunisimamia, na Team ya VPO/NEMC na Mawaziri wote kwa ushirikiano. Nampongeza @HusseinBashe na Simbachawene kwa kuaminiwa. Nawatakia heri na kuwaahidi ushirikiano wangu wa dhati. ??
— January Makamba (@JMakamba) July 22, 2019
Kumekuwa na mjadala mzito katika mitandao ya kijamii na kwenye vyombo vya habari baada ya Makamba kuondolewa katika nafasi hiyo huku baadhi wakijaribu kubashiri sababu za kuondolewa kigogo huyo katika Baraza la Mawaziri la Rais Magufuli.
Sehemu kubwa ya jumuiya ya watumiaji wa mitandao nchini wamempa pole Makamba huku wengine wakieleza kuwa kuenguliwa kwake katika uwaziri kutampa muda zaidi wa kuwatumikia wapiga kura wake jimboni.
Makamba alikuwa ni miongoni mwa mawaziri wachache ambao hawajawahi kuguswa na Dk Magufuli tangu aunde baraza lake la mawaziri mwishoni mwaka 2015.
Hata hivyo, katika hotuba yake leo baada ya kuwaapisha mawaziri hao wapya, Rais Magufuli aligusia kidogo baadhi ya masuala katika wizara ya Muungano na Mazingira ambayo huenda ni moja ya sababu ya Makamba kung’olewa ikiwemo usimamizi mbovu wa fedha za miradi ya mazingira kutoka kwa wafadhili na ucheleweshaji wa vibali vya mazingira vinavyotolewa na Baraza la Taifa la Mazingira (Nemc) kwa wawekezaji.
Latest
