Kodi ya majengo kuanza kukusanywa kupitia luku Agosti 20

August 19, 2021 7:39 am · Medlini
Share
Tweet
Copy Link
  • Kodi hiyo itakusanywa kupitia mfumo wa ununuzi wa umeme (luku)
  • Utaanza kutumika kesho Agosti 20, 2021.
  • Kodi ya majengo nayo yapanda kwa viwango tofauti.

Dar es Salaam. Serikali imesema utaratibu mpya wa ulipaji wa kodi ya majengo kupitia mfumo wa ununuzi wa umeme (luku) utaanza kesho Agosti 20, 2021 huku kukiwa na ongezeko la kodi hiyo.

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Alphayo Kidata amesema utekelezaji huo unafanyika chini ya usimamizi wa TRA kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ukihusisha mita za aina zote za umeme.

“Hili linafanyika kufuatia marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Sura ya 289 iliyopitishwa na Bunge la Bajeti la mwaka 2021 ambapo viwango vya kodi ya majengo vimebadilishwa,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Kidata iliyotolewa leo Agosti 19, 2021.

Wamiliki wa nyumba za kawaida ndani ya kiwanja kimoja watalipa Sh12, 000 badala Sh10, 000 iliyokuwa ikitozwa awali na Sh60,000 kwa kila sakafu ya ghorofa kutoka Sh50,000 kwa mwaka.

Hata hivyo, halmashauri za wilaya na miji midogo, nyumba za ghorofa bila kujali idadi ya sakafu wao watalipa Sh60,000. 

Kwa utaratibu huo mpya wa ukusanyaji wa kodí, kíla mnunuzi wa umeme atakatwa Sh1,000 kwa mwezi kwa nyumba ya kawaida na Sh5,000 kwa mwezi kwa kila sakafu ya ghorofa.

Kwa wanaotumia mita za ankara watalipa kodi hiyo kwa pamoja katika ankara ya mwezi, ameeleza Kidata katika taarifa hiyo. 

“Kwa wamiliki ambao majengo yao hayajapata umeme, wataendelea kulipa kodi hiyo kwa kutumia mfumo uliokuwa unatumika hapo awali ambao ni njia ya simu ya mkononi na benki baada ya kupata namba ya kulipia malipo (Control Number) mpaka hapo watakapoingiziwa umeme,” imeeleza taarifa hiyo.

Aidha, wamiliki wa majengo na wananchi watakaokatwa kodi hiyo kimakosa na wale watakao kuwa na malalamiko mbalimbali, watatakiwa kufika katika ofisi za TRA zilizo karibu na maeneo yao kwa ajili ya kushughulikiwa.

Hapo awali Kodi ya Majengo ilikuwa ikikusanywa na mamlaka za Serikali za mitaa ambapo mwaka 2016/17 jukumu hili lilihamishiwa TRA na hadi sasa mamlaka hiyo inaendelea kulitekeleza.

Huenda utaratibu huo mpya ukasaidia kuongeza kasi ya ukusanyaji kodi hiyo ya majengo katika maeneo mbalimbali nchini.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW