Serikali yafafanua madai ya kisiwa cha Lupita kuuzwa
- Yasema kisiwa hicho hakijauzwa kama ardhi kwa mwekezaji binafsi.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imekanusha kuuzwa kwa Kisiwa cha Lupita, ikisema eneo hilo limekodishwa kwa kampuni ya Firelight Safaris Ltd kwa ajili ya uwekezaji na haki hiyo inaweza kuhamishiwa kwa mwekezaji mwingine kwa mujibu wa sheria.
Ufafanuzi huo umetolewa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi baada ya kusambaa kwa taarifa kupitia mitandao ya kijamii na vyombo vya Kimataifa kwamba bilionea wa Marekani, Tim Draper, anatafuta mnunuzi wa kisiwa hicho kilichopo Ziwa Tanganyika, Wilaya ya Nkasi, Mkoa wa Rukwa.
Taarifa hiyo aliyochapisha Draper mwenyewe kupitia mtandao wake wa X Agosti 28, 2026 na kuripotiwa na jarida la Marekani la Forbes, Agosti 29, 2026 ilizua mjadala kwenye mitandao ya kijamii kuhusu uhalali wa mwekezaji huyo kuuza kisiwa hicho.
Taarifa ya Draper ilisema kuwa “Ninauza kisiwa changu kilichopo katika Ziwa Tanganyika, Tanzania. Ni eneo zuri sana, lakini hatulitumi vya kutosha. Bei ni Dola za Marekani milioni 7.9 (takribani Sh21.2 bilioni) au ofa bora zaidi. Yeyote anayevutiwa na ununuzi huo awasiliane nami moja kwa moja kupitia tim@draper,”.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Agosti 31,2026 na kitengo cha mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Lupita ni eneo lililotengwa kwa uwekezaji chini ya Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) na limepangishwa kwa kampuni ya Firelight Safaris Ltd, ambayo Draper ni miongoni mwa wanahisa.
Aidha, Wizara imefafanua kuwa Sheria ya Ardhi, Sura ya 113, inaeleza wawekezaji raia wa kigeni hupata ardhi kwa ajili ya uwekezaji kupitia utaratibu maalumu unaotambuliwa kisheria ikiwemo kupitia TISEZA.
“TISEZA ambao ndio wamiliki kwa mujibu wa sheria, wamepangisha eneo hilo na kutoa Hakimiliki Isiyo ya Asili (Derivative Right) kwa kampuni ya Firelight Safaris Ltd kwa matumizi ya hoteli ya kitalii,” imeeleza Wizara.
Kutokana na utaratibu huo, kampuni hiyo inaweza kuhamisha uwekezaji wake kwa mwekezaji mwingine, ikiwa uhamishaji huo utafanyika kwa kuzingatia sheria na taratibu za Tanzania.
Ufafanuzi huo unalenga kuweka wazi kuwa kinachoweza kuhamishwa si umiliki wa ardhi ya Tanzania kwa maana ya kuuza ardhi kwa mgeni, bali ni uwekezaji na haki ya matumizi ya eneo iliyotolewa kwa mujibu wa sheria.
Draper, alinunua eneo hilo, mwaka 2004 na kutumia miaka minne kulijenga, likiwa na nyumba 10 za kulala wageni, spa, chumba cha mazoezi, chumba cha michezo, baa kadhaa na bwawa la kuogelea.