Mpungwe, mwenyekiti mpya Bodi ya Wakurugenzi TBL
- Ami Ramadhan Mpungwe amechukua nafasi ya Leonard Mususa aliyefariki Mei 30, 2026 akiwa katika nafasi hiyo.
Dar es Salaam. Bodi ya Wakurugenzi ya Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL) imemteua Balozi mstaafu Ami Ramadhan Mpungwe kuwa Mwenyekiti mpya wa bodi hiyo, akitarajiwa kuchochea ukuaji wa kampuni hiyo.
Mpungwe anaingia katika nafasi hiyo akiziba pengo la Leonard Mususa, aliyefariki Mei 30, 2026, akiwa na jukumu la kutumia uzoefu na ujuzi wake kuisaidia TBL kutekeleza mikakati yake, kukabiliana na ushindani na kuendeleza ukuaji wa kampuni.Â
TBL imetangaza kumteua Mpungwe katika nafasi hiyo leo Agosti 24, 2026 ikimpongeza na kumtakia kila la heri katika majukumu yake mapya ambayo alishaanza kuyatekeleza tangu alipoteuliwa kuwa mwenyekiti wa mpito kufuatia Mkutano Mkuu wa 53 wa TBL.Â
Uteuzi huo unafungua ukurasa mpya katika safari ya kampuni hiyo, huku Mpungwe akitumia uzoefu wake katika diplomasia, uwekezaji wa sekta binafsi na uongozi wa biashara kuisaidia TBL kutekeleza mikakati yake na kuimarisha zaidi biashara yake.Â
Kutoka diplomasia hadi biashara
Kabla ya kuingia katika sekta binafsi na kuwekeza nguvu katika biashara, Mpungwe alianza safari yake ya kikazi katika utumishi wa umma, akihudumu kama mwanadiplomasia na baadaye kuwa Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini.Â
Baada ya kustaafu utumishi wa kidiplomasia, Mpungwe aliendelea kushiriki katika shughuli za sekta binafsi na uongozi, ikiwemo uteuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan mwaka 2023 kuwa mjumbe wa Tume ya Mipango.Â
Katika historia ya biashara, Mpungwe amewahi kushika nafasi mbalimbali ikiwemo Makamu Mwenyekiti Mtendaji wa Bodi ya kampuni ya TanzaniteOne ambapo alikuwa na jukumu la kusaidia kuongoza shughuli za kampuni hiyo nchini Tanzania.
Hata hivyo, Mpungwe si mgeni katika kampuni ya TBL, kabla ya kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi, alihududmu kama mjumbe wa Bodi ya TBL na na AB InBev Africa BV, kampuni inayowakilisha maslahi ya AB InBev katika kampuni hiyo tangu Oktoba 2021, jambo linalompa uzoefu wa ndani kuhusu uendeshaji, biashara na mikakati ya kampuni hiyo.
Akabidhiwa kijiti cha kukuza mapato
Uteuzi huo wa Mpungwe unaambatana na jukumu la kuendeleza ukuaji wa kampuni hiyo iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), hasa katika kuongeza thamani ya biashara na manufaa kwa wanahisa.
Kwa mwaka ulioishia Desemba 31, 2025, TBL ilirekodi mapato ya Sh1.658 trilioni, yakiongezeka kwa asilimia 13 kutoka Sh1.467 trilioni mwaka 2024.
Aidha, faida baada ya kodi iliongezeka kwa asilimia 15.8, kutoka Sh163 bilioni mwaka 2024 hadi Sh188.8 bilioni mwaka 2025.