Chalamila kutegua kitendawili cha mabasi stendi ya Magufuli
- Amesema sheria kali zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kufutiwa leseni.
- Awataka viongozi kuweka mazingira rafiki kwa wananchi.
Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ametoa onyo kali kwa wamiliki na madereva wa mabasi wanaokaidi utaratibu wa kupakia na kushusha abiria katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli akisisitiza kuwa watakaokiuka watachukuliwa hatua.
Chalamila aliyekuwa akizungumza leo Agosti 19, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa ukaguzi wa utekelezaji wa agizo alilotoa la mabasi yote yanayofanya shughuli zake nje ya stendi kuu kurejea ndani ya siku saba amesema mabasi yanayowasili Dar es Salaam yanapaswa kushusha abiria katika Kituo cha Magufuli.
“Sitaki kuona basi kwenye uso wa Shekilango na mtu yeyote atakayekaidi kuanzia hivi naavyozungumza tena nataka niwadhibitishie tutapeleka mahakamani,”ameeleza Chalamila wakati akizungumza na wananchi.
Hii si mara ya kwanza kwa viongozi wa juu katika ngazi ya mkoa kutoa onyo kali kwa mabasi yanayopakia na kushusha abiria katika vituo vingine tofauti na Kituo cha Magufuli kilichojengwa mwaka 2021 kikitumia zaidi ya Sh50 bilioni.
Miezi michache baada ya kuzinduliwa kuliibuka malalamiko kwa baadhi ya Wananchi baada ya wamiliki hao kukitosa kituo hicho kwa madai ya umbali na kutokuwepo kwa miundombinu rafiki.
Akiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati huo Chalamila alitoa onyo kali na kuagiza wamiliki hao kurejesha shughuli zao katika kituo hicho agizo ambalo halikutekelezeka mpaka alipong’oka katika nafasi hiyo.
Mei 2022, aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Innocent Bashungwa, alitoa agizo hilo hilo akimtaka aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati huo Amosi Makala kulisimamia ipasavyo hatua ambayo iligonga mwamba.
Akizungumza wakati wa ziara katika kituo hicho Chalamila amewatwisha ‘zigo’Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) na mamlaka nyingine zinazohusika kuchukua hatua kali za kisheria ikiwemo kuwafutia vibali watakaokaidi agizo hilo.
Kero kufanyiwa kazi
Chalamila amewaahidi Watanzania kuwa Serikali itafanya maboresho ya miundombinu na usimamizi wa Kituo cha Magufuli, ikiwemo kuweka maeneo maalumu kwa ajili ya kukatia tiketi na mifumo ya kisasa ya ukusanyaji wa ushuru itakayopunguza mianya ya upotevu wa fedha.
Ahadi hiyo ilipokelewa kwa shangwe na Wananchi waliokuwa katika eneo hilo kuanzia saa nne asubuhi wakisubiri ujio wa mkuu wa mkoa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Masando, amesema tayari wameanza kutekeleza maagizo hayo kwa kuhakikisha mabasi yaliyokuwa yakipakia na kushusha abiria katika maeneo ya Shekilango na Magomeni yanaelekezwa Kituo cha Magufuli kwa mujibu wa leseni za LATRA.
“Hatutaruhusu basi ambalo halijatoka Stendi ya Magufuli na halijakaguliwa kuendelea na safari yake kwa sababu linavunja sheria,” amesema Masando.
Amesema pia usalama wa kituo umeimarishwa kwa kuwepo kwa Jeshi la Polisi na ushirikiano wa vijana wa bodaboda na bajaji, huku huduma za maji na vyoo zikiboreshwa ili kuwahudumia abiria na watumiaji wengine wa kituo hicho.