Ifahamu Michembe, chakula cha asili cha kabila la Wasukuma
- Ni viazi vitamu vilivyokatwa vipande na kukaushwa ambavyo Wasukuma hutumia kama kifungua kinywa.
Dar es Salaam. Unapotaja makabila yaliyopo nchini Tanzania si rahisi kuliacha kabila la Wasukuma ambalo ni miongoni mwa makabila maarufu kati ya zaidi ya makabila 120 yaliyopo nchini.
Licha ya kuwepo karibu katika kila mkoa, asili ya kabila hili ni maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria, Kaskazini mwa Tanzania.
Kama yalivyo makabila mengine kabila hili pia lina mila na desturi zake ambazo ukiacha mambo mengine kuna vyakula vya asili ambavyo hupendelea.
Mbali na ugali dagaa ambao Wasukuma hupendelea zaidi kuna chakula kinaitwa ‘Michembe’
Michembe ni nini
Michembe ni chakula kinachotokana na viazi vitamu vilivyokatwa vipande vidogo mithiri ya ‘Crips’ lakini yenye upana kidogo kiasi ambacho haiwezi kuvunjika kirahisi, kisha vipande hivyo huanikwa juani na kukauka kaukau, kiasi ambacho hakuna mdudu ataweza kupenya, pindi vinapo hifadhiwa.
Ukiachana na Michembe kuwa chakula nyuma yake pamefichwa teknolojia ya uhifadhi wa chakula kwani Wasukuma hukausha viazi hivyo kama njia ya kuhifadhi kwa ajili ya matumizi ya baadae ikiwa wamepata mavuno mengi.
Chakula hiki ni chakula cha asili cha Wasukuma lakini kinaweza kuliwa na mtu yeyote hivyo Jiko Point leo tumekuletea makala hii kukuelekeza namna ambavyo unaweza kuandaa chakula hiki na kukifurahia.

Hatua kwa hatua jinsi ya kuandaa Michembe
Kupika michembe sio kazi kama ambavyo wadada wa mjini walivyozoea kukaanga chipsi. Hatua ya kwanza pima kiasi cha michembe kulingana na ukubwa wa familia yako au kiasi kinachokutosha ikiwa upo mwenyewe.
Michembe huwa na tabia kuvimba hivyo ni vyema kuwa muangalifu katika makadirio ya kiasi.
Kwa sababu ni chakula kinachohifadhiwa kwa muda mrefu, na huwa ni kigumu ni muhimu kuosha kwa maji safi ya uvuguvugu kabla ya kuendela na mapishi.
Kadiria kiasi cha maji kwenye sufuria kulingana na kiasi cha michembe ulichopima kisha bandika kwenye jiko lako linalotumia nishati safi ili yachemke kwa dakika chache.
Mara baada ya maji kupata moto, weka Michembe kwenye chungu ukifatia na chumvi kiasi, kisha funika na ugeuze mara kwa mara mpaka ichanganyike na kuwa kama futari.
Kupika michembe hakuna tofauti na kuchemsha viazi vya kawaida hivyo unaweza kuonja ili kujua kama Michembe yako iko tayari. Ikiwa umeonja na kujiridhisha kwamba imeiva basi unaweza kuepua chakula chako na kukiandaa tayari kwa kuliwa.
Faida za Michembe kiafya
Kwa mujibu wa Utafiti uliofanywa na Taasisi ya kilimo Tanzania (TARI) unaonesha kuwa Michembe ina virutubisho vingi kama vile wanga na nishati, vitamini A, nyuzinyuzi na protini ambazo zote husaidia kuupa mwili nguvu na hii ndio sababu wasukuma hupendelea kula chakula hiki kabla ya kazi ngumu.
Wasukuma hutumia Michembe nyakati za asubuhi kama kifungua kinywa wanapojiandaa kwenda shamba au machungani. Hata hivyo, unaweza kula chakula hiki wakati wowote na kinapendeza zaidi kushushia na kinywaji kama maziwa au chai.