Kutana na mashine inayonyoyoa kuku watatu kwa dakika moja
- Mashine hiyo inaitwa ‘Poultry Plucker’ na inaweza kunyonyoa kuku 1,440 kwa saa nane.
Dar es Salaam. Katika biashara ya kuku, kasi, ubora na ufanisi ni mambo yanayoamua mafanikio. Kila dakika inayookolewa katika uzalishaji inaweza kuongeza maokoto.
Kwa miaka mingi, wafugaji na baadhi ya wachinjaji wamekuwa wakinyonyoa kuku kwa mikono njia inayotumia muda mwingi, nguvu kazi na gharama zaidi.
Lakini sasa itakuaje kama nikikuambia kuwa unaweza kunyonyoa kuku watatu ndani ya dakika moja, yaani namanisha kila ndani ya saa moja unaweza kunyonyoa kuku 180 hivyo ndani ya saa nane za kazi mfugaji anaweza kunyonyoa kuku 1,440.
Kazi hiyo inaweza kurahisihwa ikiwa una mashine zaidi ya moja na wafanyakazi wengi, hali itakayofanya kuchakata idadi kubwa ya kuku na kuwahudumia wateja kwa haraka.
Mashine yenye kipenyo cha sentimita 50/60 ilikuwa miongoni mwa vivutio vikubwa katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam, maarufu kama Sabasaba.
Nukta TV ilikutana na mashine ya kunyonyoa kuku, maarufu kama ‘Poultry Plucker’, ambayo imevutia wafugaji, wauzaji na wafanyabiashara wengi wa kuku.
Juliana Elias ndiye muuzaji wa mashine hiyo ambapo anaeleza kuwa imekuwa mkombozi kwa wafanyabiashara wa kuku Tanzania na maeneo jirani.
“Mashine hii inanyonyoa kuku watatu hadi wanne kwa dakika moja tu, ni kwa ajili ya kuwasaidia wajasiliamali wadogo wadogo ambao wanaanza ili kuwarahisihia kazi,” anaeleza Juliana.
Ikiwa mashine hii itafanya kazi kwa saa moja mfululizo, itatumia uniti moja tu ya umeme ambayo kwa mujibu wa Mamlaka ya Nishati (EWURA) huuzwa kwa Sh292 kwa wateja wa majumbani, biashara ndogondogo, viwanda vidogo.
Kwa kiwango hicho kwa saa 8 kwa siku mashine hiyo itatumia wastani wa uniti 6 hadi 8 za umeme, kutegemeana na mzigo wa kazi sawa na Sh2,336.
Ili kupata mashine hiyo itakulazimu kutoboa mfuko wako hadi Sh1,200,000 katika mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Mwanza na Mbeya.
Kwa wafanyabiashara wadogo na matumizi ya nyumbani gharama hiyo inaweza kuwa kubwa kutokana na changamoto za mitaji.
Je, kwa uwezo wako, matumizi ya umeme na gharama iliyoelezwa na muuzaji, mashine hii inaweza kuwa suluhisho sahihi kwa biashara yako ya kuku?
Makala hii imeandikwa na Fatuma Hussein, Goodluck Gustavo na kuhaririwa na Lucy Samson