Gawio la Serikali lapaa kwa asilimia 30 lafikia Sh1.327 trilioni
- Kati ya fedha hizo, Sh800 bilioni sawa na asilimia 60 zimetokana na gawio la mashirika ya biashara.
Dar es Salaam. Serikali imekusanya Sh1.327 trilioni kama gawio na michango mingine kutoka mashirika ya umma na kampuni ambazo ina umiliki wa hisa hadi Juni 29, 2026, ikiwa ni ongezeko la asilimia 30 kutoka Sh1.02 trilioni zilizokusanywa mwaka jana.
Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu aliyekuwa akizungumza katika hafla ya Siku ya Gawio iliyofanyika leo Juni 30, 2026 Ikulu ya Dar es Salaam amesema ongezeko hilo linaonyesha matokeo ya mageuzi ya kiutendaji na kiusimamizi yanayoendelea kufanyika katika taasisi za umma.
“Ni udhibitisho kwamba taasisi za umma zinaendelea kuwa nyenzo muhimu katika kufanikisha ajenda ya maendeleo ya taifa kujenga uchumi shindani na kuharakisha utekelezaji wa dira ya 2050,” amesema Mchechu.
Mchechu ameongeza kuwa kati ya fedha hizo, Sh800 bilioni sawa na asilimia 60 zimetokana na gawio la mashirika ya biashara, Sh406 bilioni sawa na asilimia 30 zimetokana na michango ya taasisi zisizo za biashara, huku Sh121 bilioni zikitokana na vyanzo vingine vya mapato.
Aidha, Mchechu amesema utegemezi wa taasisi zisizo za biashara umeendelea kupungua kwa asilimia 12.8, hatua inayoonyesha kuimarika kwa ufanisi na usimamizi wa taasisi hizo.
Jitihada za kuongeza mchango wa mashirika ya umma katika mapato ya Serikali zilianza kupewa msukumo mwaka 2018 wakati wa utawala wa Rais wa awamu ya tano, Hayati John Pombe Magufuli alipoyaagiza mashirika yanayopata faida kutoa gawio kwa Serikali kwa mujibu wa sheria.
Baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuingia madarakani aliendeleza mkakati huo baada ya kuanzisha Siku ya Gawio ambayo ilianza rasmi Juni 11, 2024 na hufanyika kila mwaka kama jukwaa la kutathmini tija ya uwekezaji wa Serikali .
Akihutubia hafla hiyo, Rais Samia amewataka mawaziri na viongozi wa taasisi kusimamia kwa karibu utendaji wa mashirika yaliyo chini yao ili yaweze kujitegemea na kuongeza mchango wake kwa Serikali badala ya kuendelea kutegemea ruzuku.
“Natamani kuona idadi ya taasisi zinazochangia Mfuko Mkuu wa Serikali ikiongezeka sambamba na kupungua kwa utegemezi wa ruzuku kutoka Serikalini,” amesema Rais Samia
Rais Samia amebainisha kuwa, Siku ya Gawio imekuwa siku muhimu kwa wananchi kwa kuwa fedha zinazokusanywa huelekezwa katika kugharamia huduma za jamii na miradi ya maendeleo.