Tabora United yauzwa rasmi, sasa kuitwa TRA United
- TRA United itahamasisha ulipaji kodi
- Licha ya kubadilishwa jina timu hiyo itaendelea kubaki katika mkoa wa Tabora.
Arusha. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetangaza kuinunua rasmi timu ya Tabora United na sasa itajulikana kwa jina la TRA United Sports Club.
Tetesi za klabu hiyo inayoshiriki ligi kuu Tanzania Bara kuuzwa zilianza kusambaa katika mitandao ya kijamii wiki moja iliyopita ambapo zilipingwa vikali na viongozi wa timu hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa ya TRA iliyotolewa leo Septemba 19, 2025 na Idara ya Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano inabainisha kuwa baada ya taratibu za kuimiliki timu hiyo kukamilika itaendelea kusalia katika Mkoa wa Tabora kabla ya kuhamia katika jiji la Dar es salaam au Dodoma yalipo makao makuu ya taasisi hiyo ya Serikali.
Hata hivyo, taarifa huyo haijaweka wazi kuwa timu hiyo itaendelea kusalia katika mkoa wa Tabora kwa muda gani.
Katika hatua nyingine TRA imebainisha kuwa timu hiyo iliyobadilishwa jina itakuwa na majukumu mengine mbali na kutoa burudani ya mpira ambayo ni pamoja na kuhamasisha ulipaji kodi.
“Pia (klabu ya TRA United) itakuwa na malengo mbalimbali ikiwa ni pamoja na yafuatayo, kuhamasisha ulipaji kodi wa hiari, kutoa elimu ya masuala ya kodi na umuhimu wa kulipa kodi, ueneza ujumbe wa uzalendo na uwajibikaji wa kodi kwa maendeleo ya Taifa…
…Kuendeleza vipaji vya michezo nchini, kuimarisha uwajibikaji wa kijamii kupitia michezo kwa kuongeza ajira kwa Watanzania katika sekta ya mpira wa miguu kama inavyofanyika na timu za mpira wa miguu za Mamlaka za Mapato katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (Corporate Social Responsibility),” imesema taarifa ya TRA.
Aidha, TRA imewataka wadau wote wa michezo na Watanzania kwa ujumla kuiunga mkono timu hiyo ili kutimiza azma ya Taifa ya kujenga uchumi imara kupitia ulipaji wa kodi wa hiari.
TRA sio timu ya kwanza inayomilikiwa na taasisi kushiriki Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara, tayari kuna timu kama JKT Tanzania inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa, Tanzania Prisons inayomilikiwa na Jeshi la Magereza pamoja na timu zinazomilikiwa na manispaa kama Kinondoni, Dodoma pamoja na Mbeya.