Unywaji wa maziwa bado bado Tanzania
- Mwenyekiti wa DTB asema kiwango kidogo cha unywaji wa maziwa husababisha udumavu kwa watoto.
- Awataka wachakataji maziwa kusogeza huduma hiyo karibu na wananchi.
Mwanza: Mwenyekiti wa Bodi ya Maziwa (DTB), Zacharia Masanyiwa amesema unywaji wa maziwa bado ni tatizo kwa watu wengi nchini jambo linalosababisha baadhi yao ikiwemo watoto kukosa virutubisho muhimu vinavyojenga mwili.
Masanyiwa aliyekuwa akitembelea kiwanda cha uchakataji wa maziwa kilichopo Mecco mkoani Mwanza leo Mei 28, 2024 amesema bodi hiyo ni miongoni mwa wadau muhimu katika kuhamasisha unywaji wa maziwa nchini ili kukabliana na udumavu.
“Bodi ya Maziwa ni miongoni mwa wadau muhimu katika sekta ya afya kwa kuhamasisha unywaji wa maziwa ili kukabiliaiana na tatizo la udumavu kwa watoto nchini,” amesema Masanyiwa.
Soma zaidi: Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania
Kauli hiyo ya Masanyiwa inakuja wakakati Tanzania ikiadhimisha wiki ya maziwa iliyoanza leo na kilele chake kitafanyika Juni Mosi, 2024 jijini Mwanza.
Bodi hiyo imetumia wiki ya maziwa kugawa kinywaji hicho katika Hospitali ya Nyamagana na kituo cha kuelelea watoto cha Hope village kilichopo mkoani Mwanza ambapo pia imeagiza wachakataji wa maziwa kuweka dirisha maalum la kuuza kiywaji hicho maeneo ya hospitali ili kuongeza hamasa ya unywaji wa maziwa kwa wananchi.
Baadhi ya wakazi jijini Mwanza wameeleza sababu zinazochangia wao kutokunywa maziwa ni ukosefu wa fedha kwa kuwa maziwa yanauzwa ghali na hayapatikani kirahisi.