Umoja wa Ulaya watoa Sh275.8, milioni kusaidia waathirika wa mafuriko Tanzania
- Zinajumuisha utoaji wa chakula, maji, usafi wa mazingira, na huduma za afya.
- EU yaahidi kuendelea kushirikiana na Watanzania muda wote wa nyakati ngumu.
Dar es Salaam. Umoja wa Ulaya (EU) umetoa Euro 100,000 sawa na Sh275.8 milioni kusaidia waathirika wa mafuriko katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania ukiwemo mkoa wa Manyara ambako maporomoko ya matope yalisababisha vifo vya watu 89 na majeruhi zaidi ya 130.
Taarifa iliyotolewa na Kelvin Mutagwaba, ambaye ni Afisa Mawasiliano wa EU jijini Dar es Salaam leo Januari 4, 2024 imebainisha kuwa msaada huo utatumika kulisapoti Shirika la Msalaba Mwekundu linaloendelea kutoa usaidizi katika kaya 44,000 zilizoathirika na mafuriko katika mikoa ya Manyara, Dar es Salaam, Kigoma, Geita na Unguja.
Mvua kubwa za El’ Nino zilinyesha katika baadhi ya mikoa nchini Tanzania hususan katika kipindi cha miezi miwili iliyopita, jambo lililosababisha kutokea kwa mafuriko katika maeneo hayo.

Mutagwaba amebainisha kuwa msaada huo wa EU, utajumuisha utoaji wa chakula, maji, usafi wa mazingira, usafi, makazi, huduma za afya na ulinzi.
“EU inaungana na Watanzania katika kipindi hiki kigumu na itaendelea kushirikiana na Watanzania kukabiliana na majanga yoyote ya kiutu siku zijazo,” amesema Mutagwaba.
Disemba 10, 2023 Rais Samia alipokea Sh2.1 bilioni za misaada kwa waathirika wa mafuriko Hanang ikiwa ni mchango kutoka mashirika 270 ya umma ambapo alieleza dhamira ya Serikali kuwajengea nyumba wakazi waliobomolewa nyumba zao kutokana na maafa yaliyotokea.
Kwa mujibu wa Rais Samia kaya 107 zenye wakazi 332 ndio zilizopoteza makazi ambapo Serikali iliahidi kuwajengea nyumba wakati wakiishi kwenye makazi ya muda.
Latest