Mambo yatakayosaidia kupunguza magonjwa yasiyoambukiza
Mwenyekiti wa Chama cha ugonjwa wa Kisukari Tanzania Profesa Andrew Swai, akiwasilisha mada katika mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uelewa wa waandishi wa habari kutoka mikoa ya Kanda ziwa namna ya kuripoti habari zinazohusu magonjwa yasiambukiza yaliofanyika jijini Mwanza. Picha | Mariam John.
- Ni pamoja na watu kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi.
- Kula mlo kamili na kuepuka tabia hatarishi za unywaji pombe.
Mwanza. Watanzania wametakiwa kujenga tabia ya kufanya mazoezi angalau dakika 30 kwa siku ili kupunguza hatari ya kupata magonjwa yasiyo ya kuambukiza ambayo yanachangiwa na kutokuushughulisha mwili.
Pia wametakiwa kuzingatia aina ya ulaji wa vyakula vya asili na kupunguza matumizi ya pombe na uvutaji wa tumbaku ambavyo vinatajwa kuchangia kwa kiasi kikubwa kwa magonjwa hayo.
Mwenyekiti wa Chama cha Ugonjwa wa Kisukari Tanzania, Profesa Andrew Swai amesema magonjwa yasiyo ya kuambukiza hayana vimelea vinavyoweza kusambazwa isipokuwa hutokea kutokana na uzembe wa mtu au kurithi.
Ameyataja magonjwa hayo kuwa ni saratani, magonjwa sugu ya njia ya hewa, kisukari, magonjwa ya akili, ajali pamoja na selimundu.
“Magonjwa haya yameendelea kuongezeka kwa kasi ambapo takwimu zinaeleza kuwa asilimia 71 ya vifo vyote duniani kwa mwaka 2016 vilitokana na magonjwa hayo huku asilimia 75 ya vifo vyote kwa watu wenye miaka 30-70 husababishwa na magonjwa hayo,” amesema Prof Swai.
Profesa Swai ameeleza visababishi vya magonjwa hayo kuwa ni pamoja na ulaji usiofaa na matumizi ya vilevi, tumbaku, kutoshughulisha mwili, msongo wa mawazo na kutopata usingizi wa kutosha.
Mratibu wa magonjwa yasiyoambukiza kutoka Wizara ya Afya Shadrack Buswelu, amesema magonjwa hayo mbali na kifo yanaweza kusababisha ulemavu mfano kisukari kinaweza kusababisha mtu kuwa kipofu na kukatwa viungo vya mwili.
Baadhi ya viungo kushindwa kufanya kazi na kushindwa kufanya mapenzi ipasavyo huku akisisitiza kuwa wagonjwa hao ikiwemo wa kisukari kuzingatia ulaji bora wa chakula ikiwemo vyakula vya wanga.
Dk Waziri Ndonde kutoka shirikisho la vyama vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania, amewaomba waandishi wa habari kuelimisha jamii juu ya magonjwa yasiyoambukiza.
Dkt Ndonde, amesema amewataka watu kujenga tabia ya kufanya mazoezi angalau kwa dakika 30 kwa siku.
Latest
