Wanafunzi zaidi ya 27,000 waliokosa mikopo kusajiliwa vyuo vikuu
- Serikali yasema itawapa mikopo wanafunzi 28,000 wenye vigezo.
- Walikosa mikopo watakiwa kuendelea na taratibu za usajili kwa maelekezo kutoka bodi ya mikopo.
Dar es salaam. Huenda matumaini ya kusoma elimu ya juu yakarejea kwa baadhi ya wanafunzi walioshindwa kujisajili katika vyuo walivyodahiliwa, mara baada ya Serikali kuonesha nia ya kutaka kugharamia masomo yao kupitia mikopo ya elimu ya juu.
Wanafunzi hao wametakiwa kuendelea na taratibu za usajili katika vyuo walivyochaguliwa kwani Serikali inaandaa utaratibu wa kuwapa mikopo hiyo.
Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa aliyekuwa akihitimisha shughuli za Bunge hii leo Novemba 11,2022 bungeni jijini Dodoma, amewaambia wabunge kuwa Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia wanafunzi waliokosa mikopo kuendelea na hatua za usajili kwa kufuata mwongozo wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (Heslb).
“Wanafunzi wote waliokidhi vigezo vya kupata mkopo waende vyuoni kuendelea na usajili kwa maelekezo ya bodi ya mikopo, lengo la Rais ni kuwanufaisha wanafunzi wote wenye uhitaji, waliopata udahili na wenye vigezo vya kupata mikopo,” amesema Majaliwa.
Hatua hiyo inakuja zikiwa zimepita siku chache tu tangu Bunge lilipojadili hoja ya ugharamiaji, upangaji, utoaji na urejeshaji wa mikopo ya elimu ya juu mara baada ya wanafunzi takribani 28,000 wenye uhitaji kutopangiwa mikopo kutokana na ukomo wa bajeti.
Soma Zaidi
Majaliwa ameongeza kuwa Serikali itaomba Bunge liridhie matumizi ya fedha zitakazohitajika kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi hao wakati wa mapitio ya bajeti ya nusu ya mwaka.
HESLB ilipanga kutoa mikopo yenye thamani ya kiasi cha Sh570 bilioni kwa mwaka wa masomo 2022/23 ambayo imeonekana kutotosha.
Kutokana na malalamiko juu ya ufanisi wa HESLB, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda aliunda tume ya wataalamu ambao watachunguza ufanisi wa bodi hiyo katika ugharamiaji wa elimu ya juu kwa wahitaji.
“Serikali imeyapokea maazimio ya Bunge yaliyotokana na taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu kuifanyia ukaguzi wa kina Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu,” amesema Majaliwa.