Barrick yatoa zaidi ya Sh70 bilioni kwa Tanzania kujenga miundombinu ya elimu
- Zitasaidia kujenga zaidi ya madarasa 1,094 na mabweni 256 ya kidato cha tano na sita.
- Zitatolewa kwa awamu tatu ambapo awamu ya kwanza wameshatoa Sh23.3 bilioni.
- Rais Samia awaomba wadau wengine kumuunga mkono.
Dar es Salaam. Kampuni ya madini ya Barrick Gold imeipatia Tanzania na Dola za Marekani milioni 30 (Sh70.2 bilioni) kwa ajili ya shughuli mbalimbali za elimu ikiwemo kujenga madarasa pamoja na mabweni.
Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliyekuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa mradi wa kilimo wa mashamba ya pamoja (block farming ) ametoa taarifa hiyo alipokuwa akiomba radhi mara baada ya kuchelewa kufika katika hafla hiyo
“Niwaombe radhi kabla ya kuja hapa nimechelewa kidogo, nilikuwa napokea cheki ya Dola milioni 30 kutoka mgodi wa Barick na hii ni kwa ajili ya madarasa ya wanafunzi, na niwaombe wengine waje watuunge mkono,” amesema Rais Samia.
Kwa mujibu wa Rais Samia fedha hizo zinatarajiwa kusaidia ujenzi wa madarasa zaidi ya 1,094 pamoja na mabweni 276 kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano na sita katika sehemu mbalimbali nchini.
Soma zaidi
-
Rais Samia: Nendeni mkafanye kilimo biashara tuongeze tija Tanzania
-
Rais Samia : Tanzania itakuwa ghala la chakula barani Afrika
- Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano mkubwa wa Afrika wa chakula na kilimo
Zaidi ya wanafunzi 72,000 wanatarajiwa kuhitimu kidato cha sita Mei mwaka huu huku zaidi ya wanafunzi 192, 000 wakitarajiwa kuanza kidato cha tano Julai mwaka huu.
“Hiyo ndiyo kazi inayoninyima usingizi kwa sasa mpaka Julai kuhakikisha watoto wangu wa kidato cha tano wote wanaingia madarasani, “ amesema Rais Samia.
Rais Samia ametumia fursa hiyo kuwaomba wadau wengine wa maendeleo kumshika mkono katika suala hilo kwani pamoja na Barick kutoa fedha hizo zitatolewa kwa awamu tatu ambapo wameanza na Dola za Marekani milioni 10 ambazo ni sawa na Sh23.3 bilioni za Tanzania.
Mwaka 2017 kampuni hiyo ambayo ni mmiliki wa kampuni ya Acacia iliingia kwenye mzozo na Serikali ya Tanzania juu ya usafirishaji wa mchanga wa madini au makinikia kwa kudaiwa kukwepa kodi na kuminya haki za binadamu.
Kutokana na hilo mwaka 2019 Serikali ya Tanzania iliingia ushirikiano na kampuni ya Barick ya kuunda kampuni ya madini ya Twiga ambapo Tanzania inamiliki hisa kwa asilimia 50.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea mfano wa hundi yenye thamani ya Dola za Marekani (USD) 30,000,000.00 kutoka kwa Mtendaji Mkuu ambaye pia ni Rais wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Mark Briston pic.twitter.com/qjjZg1a4CZ
— ikulu_Tanzania (@ikulumawasliano) March 20, 2023