Serikali kufanya kampeni ya ‘mlango kwa mlango’ kuhamasisha utalii wa ndani

September 2, 2021 6:43 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Itawafikia Watanzania katika nyumba zao. shuleni na ofisini.
  • Lengo ni kuongeza idadi ya watalii na mapato.

Mwanza. Serikali imesema itaanza kampeni ya mlango kwa mlango ili kuhamasisha Watanzania kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo maeneo mbalimbali Tanzania ili kuongeza wigo wa mapato. 

Sambamba na hilo itaendelea kuboresha na kuimarisha vivutio vya utalii wa ndani ikiwemo fukwe, bahari  pamoja na kutangaza vivutio vipya ili kuhakikisha inaongeza ukusanyaji wa mapato.

Afisa Masoko wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Kanda ya Ziwa, Rhoda Michael akizungumza kwenye maonyesho ya 16 ya wafanyabiashara wa Afrika Mashariki (TCCIA) amesema watafanya kampeni hiyo kuwafikia Watanzania katika nyumba zao ili kuongeza watalii wa ndani.

“Pia tunatumia maonyesho kama haya ili kutangaza vivutio vyetu hususan hivi vipya ili vijulikane kwa watanzania wengi, tutafanya kampeni mlango kwa mlango , ofisi kwa ofisi ili ili kuhamasisha watalii wa ndani,” amesema Rhoda.

Mbali na kampeni hiyo pia watatumia hamasa na elimu kwa taasisi za elimu ikiwemo shule na vyuo, pamoja na taasisi zingine ili wahamasike kutembelea vivutio vilivyopo nchini.

Kwa sasa Tanzania ina hifadhi za Taifa 22 baada ya kuanzishwa kwa hifadhi sita mpya za Nyerere, Burigi-Chato, Ibanda-Kyerwa, Kigosi, Mto Ugalla na Rumanyika-Karagwe.

Awali, Afisa uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (Tanapa), Themistiocles Bitta amesema baada ya ugonjwa wa corona uliosababisha nchi nyingi kufunga mipaka yake ulisababisha kupungua kwa idadi ya watalii waliokuwa wanatoka nje ya nchi, hivyo wameanza mikakati ya kuhamasisha utalii wa ndani.

Waziri wa Maliasili na Utalii Damas Ndumbaru katika hotuba yake ya bajeti ya 2021/22 alisema kuwa mwaka 2020 baada ya janga hilo kuingia waliweka makisio ya watalii milioni 1.8 lakini baada ya janga hilo kuingia mwezi April waliweka makisio mengine ya watalii 437,000 ambao wangetembelea hifadhi mbalimbali nchini.

Hata hivyo, ni watalii 620,867 ndiyo walioingia Tanzania mwaka jana.

“Kwa sasa tumejikita zaidi kuhamasisha watalii wa ndani ili kujenga uchumi wa kwetu na si kutegemea watalii wa nje pekee hasa katika kipindi hiki ambapo majanga makubwa kama haya yanatokea,” amesema Bitta.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW