Google kumwaga mabilioni kwa startups za Afrika

October 7, 2021 7:14 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Itawekeza Sh115.2 bilioni kwa startups za bara hilo.
  • Lengo ni kutoa mitaji itakayosaidia startups zikoe na kutoa huduma.
  • Pia itawezekza Sh2.3 trilioni kwa miaka mitano ijayo barani humo.

Dar es Salaam. Kampuni ya teknolojia ya Google ya Marekani imetenga Sh115.2 bilioni kwa ajili ya kusaidia kampuni zinazochipukia (startups) zilizopo barani Afrika ili kuzisaidia kukuza biashara zao na kutoa suluhu kwa matatizo ya jamii. 

Kiasi hicho cha fedha ni sehemu ya Sh2.3 trilioni za mfuko wake wa uwekezaji barani Afrika ambazo itazitumia kwa miaka mitano ijayo katika kampuni za teknolojia barani humo.  

Mkurugenzi Mtendaji wa Alphabet Inc, kampuni ya mama ya Google, Sundar Pichai amesema lengo kutoa Sh115.2 bilioni ni kuinua biashara ndogo ndogo na startups ili kuongeza wigo wa biashara katika bara la Afrika.

Utoaji wa fedha hizo na mambo mengine unafanyika chini ya programu ya Google (Startups Accelerator Africa program). 

Hadi sasa, Startups 50 zimechaguliwa kushiriki kwenye programu hiyo ya Afrika inayotarajiwa kuanza Oktoba 13 mwaka huu ambapo kila startup itapatiwa Sh230 milioni pamoja na mikopo kutoka programu za Google za ‘Google Cloud’ na ‘Google Ads’.

Kati ya startup 50 zilizochaguliwa, asilimia 40 zinaongozwa na wanawake zikiwakilisha nchi tisa na sekta 12.

“Kuna pengo kubwa katika upatikanaji wa mitaji. Makundi mengine hayafikiwi na mitaji kama mengine. Tumeyaona hayo kwa startups zinazoongozwa na waanzilishi wanawake wenye asili ya Afrika,” amesema Mkurugenzi Mtendaji wa Google wa nchi  za Kusini mwa Jangwa la Sahara, Nitin Gajria.

Gajria amesema kuwa jitihada zinafanyika kwa ajili ya kuziba pengo hilo  na wameamua kuleta mitaji barani Afrika.

Licha ya kuwa Afrika ina nchi kubwa zilizoendelea kiteknolojia (Nigeria, Kenya, Afrika Kusini na Misri), kampuni hiyo imesema itaendelea kupokea maombi kutoka kwa startups hata katika nchi ambazo hazifikiwi na mitaji hiyo.

Nchi hizo ni pamoja na Algeria, Botswana, Cameroon, Ivory Coast, Ethiopia, Ghana, Morocco, Rwanda, Senegal, Tanzania, Tunisia, Uganda na Zimbabwe.

“Hatufungamani na nchi zozote. Tumeweka umakini wetu kwenye kuwekeza kule tunaamini Google itaongeza thamani,” amesema Gajria.

Google ambayo imekuwa ikisaidia kampuni changa kupitia Mfuko wa Uwekezaji Afrika kwa miaka mitatu sasa, imefikia startups 80 mbalimbali barani Afrika zikiwemo Twiga, Paystack na Piggyvest.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW