Mwanza ilivyojipanga kupunguza watoto wa mitaani
Viongozi kutoka idara mbalimbali wakiwa kwenye kikao cha pamoja kujadili mikakati ya kupunguza idadi ya watoto wa mitaani na njia za kukomesha utoro mashuleni. Picha| Mariam John.
- Yaandaa kampeni ya miezi miwili kuwarudisha shule.
- Kuboresha mazingira ya kusomea kuvutia wanafunzi.
- Wazazi, jamii watakiwa kuwajibika na malezi ya watoto.
Mwanza. Serikali mkoani Mwanza kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wameazimia kufanya operesheni kabambe katika mitaa na vijiji vya mkoa huo itakayosaidia watoto wote kuwepo shuleni ili watimize ndoto zao za elimu.
Operesheni hiyo ya miezi miwili itaenda sambamba na kuwaondoa watoto wanaozagaa mitaani kuhakikisha wanarudishwa shuleni.
Maadhimio hayo yamefanyika leo April 8 kwenye kikao kazi cha Kamati ya Kupambana na Ukatili wa Kijinsia kwa Wanawake na Watoto (MTAKUWA) ngazi ya Mkoa ambacho kililenga kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuwaondoa watoto mitaani na kutokomeza utoro mashuleni.
Akizungumza kwenye kikao hicho, Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ngusa Samike amewataka wadau kuwasaidia wazazi kupata elimu ya umuhimu wa mtoto kwenda shule, jambo litakalosaidia kupunguza idadi ya watoto wa mitaani.
“Katika mpango huu jambo la muhimu ni kuwaelimisha wazazi wasiwe chanzo cha watoto kuwa mitaani kwa sababu tatizo lililopo ni wazazi kuwa chambo kwa watoto wao katika kuwapanga na kuwafundisha maneno ya uongo ya kusema na wanapofuatiliwa huwahamishia sehemu nyingine,” amesema Samike.
Amesema Serikali inatoa fedha nyingi kwa ajili ya elimu bila malipo ambapo hivi karibuni Mkoa wa Mwanza ulipokea Sh20.5 bilioni kwa ajili ujenzi wa vyumba vya madarasa na madawati hivyo si vyema watoto wakakosa haki ya kupata elimu.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika lisilo la kiserikali la Kivulini, Yassin Ally amesema changamoto ya watoto mitaani inachangiwa na suala la utoro mashuleni.
Mkurugenzi huyo alishauri walimu kuwa na mbinu rafiki kwa wanafunzi za ufundishaji ikiwa ni pamoja na kupunguza adhabu kali kutokana na kukosa sare za shule au kufeli mitihani.
Yassin ameeleza kuwa tathimini iliyofanyika mwaka 2017 na Idara ya Maendeleo ya jamii kwa mikoa sita inaonyesha jiji la Mwanza ni la pili kwa kuwa na idadi kubwa ya watoto wa mitaani waliokadiriwa kufikia 978.
Mkoa unaoongoza ni Dar es Salam kwa watoto 2,684, Iringa (954), Mbeya (586) na Dodoma watoto 346.
Zinazohusiana:
-
Ukosefu wa mtaala changamoto inayogharimu watoto wenye uziwi Tanzania
-
Unayoweza kumfundisha mtoto kutumia vizuri fedha
-
Falsafa ya michezo kuboresha elimu, afya ya watoto
Akitoa taarifa ya hali ya utoro katika shule za msingi na sekondari mkoani Mwanza, Kaimu Afisa Elimu Watu Wazima na Elimu je ya Mfumo Rasmi, Maenda Chambuku amesema katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi April mwaka huu jumla ya watoto watoro 19,133 wameripotiwa shule ya msingi huku shule ya sekondari ikiwa na watoto 7,594.
Amesema Serikali imeweka mifumo rafiki kwa wanafunzi ambao hawako shuleni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mimba na utoto kurejea shuleni hivyo jitihada zifanyike ili kuhakikisha kila mtoto anapata haki ya kwenda shule.
“Utoro ni sehemu ya watoto waliopo mitaani ni jukumu letu kila mmoja kuhakikisha wanawaelimisha wazazi waweze kupunguza tatizo hilo,” amesema Chambuko.
Hata hivyo, Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza, Isack Ndassa amesema zaidi ya asilimia 90 ya watoto walio mitaani wana umri wa kwenda shule lakini wanakosa haki ya kupata elimu kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ukosefu wa uangalizi wa wazazi.