Wamarekani waunda kifaa cha kuwasaidia wanaokoroma usingizini
- Ni kifaa chenye kusaidia mfumo wa upumuaji mtu akiwa kwenye usingizi mzito.
- Umuhimu wa kifaa hicho kinasaidia mtu kupumua vizuri bila shida pindi anapokuwa kwenye usingizi.
Dar es Salaam. Usingizi ni kitu chenye kuleta afya kwa kila binadamu anaeishi ila namna tunavyolala inatofautiana kulingana na tunavyoweza kuingiza na kutoa pumzi wakati wa kulala.
Kulala kwa kukoroma kunaweza kusababishwa na ugumu wa kupumua kipindi mtu anapokuwa usingizini au matatizo katika mfumo wa kupumulia katika pua za mtu na kumsababishia kuwa na desturi ya kukoroma pindi anapokuwa kwenye usingizi mzito.
Hali hii huwa kero pale mtu anapokuwa jirani na mwenzie na kusikika akikoroma anapokuwa amelala licha ya kutokujijua kwa sababu anakuwa kwenye usingizi mzito.
Kumalizia tatizo hilo, Wamarekani wamegundua kifaa kinachoitwa Silent Snore kinachosaidia mtu anapokuwa usingizini asisikike kama anakoroma usiku mzima mpaka anapoamka kutoka usingizini.
Kifaa hicho kinafanya kazi kwa kupachikwa kwenye pande zote mbili za pua. Baada ya kukiweka puani kinasaidia mtu kuwa na uwezo mkubwa wa kupumua vizuri bila shida akiwa usingizini hata kama ana desturi ya kukoroma.
Silent Snore inasaidia kupunguza kero ya kukoroma na kuweka mdomo kwenye hali nzuri kwani inasababisha mtu kufumba mdomo pindi anapokuwa amelala kutoana na kifaa hicho kinachowekwa puani.
Kifaa hicho pia kinamweka mtu huru pindi anapokuwa amelala kujua kwamba amelala bila kusumbua watu kwa sauti za kukoroma tofauti na pale anapokuwa hajatumia kifaa hicho usingizini.
Charles Msinde, Daktari katika hospitali ya Mama Ngoma anasema kifaa hicho kinaweza kuwa na umuhimu wa kumsaidia mtu katika ulalaji wake lakini vilevile inaweza kuwa na athari kiafya kwani kinazuia upumuaji unaotakiwa.
“Hakiwezi kuwa effective (fasaha) kwa asilimia 100 kwani ukikibana kwenye pua maana yake kuna mifumo fulani inazuiliwa kutoa hewa pindi mtu anapokuwa usingizini. Hivyo si cha kukizoea sana,” amesema Msinde.
Kifaa hicho kinadaiwa kuwa ni cha kwanza kuletwa kwa ajili ya kuzuia upumuaji mgumu mtu akiwa usingizini na kinatarajia kufika Tanzania karibuni kwa matumizi kwa watu wenye uhitaji na matatizo hayo wakati wa kulala.
Latest