Uzalishaji maua, viungo mwendo wa kinyonga
- Bado uzalishaji wa maua na viungo uko chini jambo linalotoa fursa kwa vijana kutumia ardhi iliyopo nchini kuongeza uzalishaji na kufaidika na fursa zilizopo kwenye mazao hayo.
- Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki yafungua milango kwa wazalishaji kupata mafunzo Israel.
Dar es Salaam. Licha ya uzalishaji wa mazao ya matunda kuongezeka, bado uzalishaji wa maua na viungo uko chini jambo linalotoa fursa kwa vijana kutumia ardhi iliyopo nchini kuongeza uzalishaji na kufaidika na fursa zilizopo kwenye mazao hayo.
Mazao ya bustani yanajumuisha matunda, mboga, maua na viungo vinavyotumika katika shughuli za mapishi. Maua na viungo ni miongoni mwa bidhaa zinazosafirishwa zaidi katika masoko ya nje ya nchi.
Kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa katika mwaka 2017 kilichotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kinaeleza kuwa mwaka 2017 uzalishaji wa mazao ya bustani uliongezeka kwa asilimia 10.7 ikilinganishwa na asilimia 5.3 iliyorekodiwa mwaka 2016.
“Hii ilitokana na kuhamasika kwa wakulima kuongeza uzalishaji kufuatia uwepo wa soko la uhakika, kuongezeka kwa usindikaji wa mazao hayo 137 na kuongezeka kwa ulaji wa matunda na mboga,” inasomeka sehemu ya kitabu hicho.
Hata hivyo, uzalishaji wa maua na viungo uko chini zaidi ukilinganisha na mboga na matunda.
Mathalani katika kipindi hicho wakulima walizalisha tani 11,615 tu za maua ambapo ni chini zaidi mara 451 ya uzalishaji wa matunda ambao ulikuwa tani milioni 5,243,343.

Kutokana na mahitaji ya maua na viungo kuongezeka kimataifa, vijana wanaweza kutumia fursa ya kutumia ardhi iliyopo kuongeza uzalishaji na kupata fursa ya masoko ya nje.
Zinahusiana:
- Ripoti: Tanzania ni miongoni mwa nchi 11zinazowekeza kwenye utafiti wa GMO Afrika
- Rasmi: Tabora ndiyo ‘makao makuu’ ya kuku wa kienyeji Tanzania
Kutokana na umuhimu wake, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki leo (Machi 29, 2019) imetangaza mafunzo ya vitendo (field attachment) kwenye mashamba makubwa ya mazao mbalimbali yakiwemo ya matunda, mbogamboga, ufugaji, uvuvi na mazao mengine ya biashara kwa ujira maalum nchini Israel
Mafunzo hayo ya miezi 11 kuanzia Septemba, 2019 ni utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na Serikali ya Israel kwa Tanzania ili kuwaongezea ujuzi Watanzania wenye nia ya kuwekeza katika sekta ya kilimo.