Utafiti: Watanzania hawa wanatamani kumiliki nyumba, shamba lakini hawana fedha
- Ripoti ya utafiti wa masuala ya kifedha ya Finscope inasema asilimia 59 wana matamanio ya kumiliki rasilimali hizo lakini hawana fedha
- Changamoto za kipato huwakwamisha kununua nyumba na ardhi.
- Ni asilimia moja tu ya Watanzania ndiyo hawawezi kununua simu.
Dar es Salaam. Wakati ardhi na nyumba vikiwa rasilimali muhimu kwa ajili ya makazi na shughuli za maendeleo, imebainika kuwa zaidi ya nusu ya Watanzania wanapenda kumiliki rasilimali hizo lakini hawana uwezo wa kuzipata kutokana na changamoto za kipato.
Ripoti ya utafiti wa masuala ya kifedha ya Finscope ya mwaka 2017 inaeleza kuwa asilimia 40 au sawa na watu wanne kati ya 10 wanapenda kununua nyumba kwa ajili ya kuishi lakini hawana uwezo wa kufanya hivyo.
Licha ya kuwa nyumba ni chaguo la kwanza la Watanzania, asilimia 19 nao wanapenda kununua ardhi au mashamba kwa shughuli mbalimbali lakini mfuko hauruhusu. Hii ni sawa na mtu mmoja kati ya watano anayependa kununua ardhi au shamba lakini kibubu kinamkwamisha.
Kwa rasilimali zote mbili yaani nyumba na ardhi ambazo zimetaajwa na utafiti huo uliofanywa kati ya Aprili na Julai 2017 zinaunda asilimia 59 ya Watanzania ambao wana matamanio ya kuzinunua lakini hawawezi.
Matamanio hayo ya Watanzania huyeyuka kutokana na changamoto ya kipato na kuongezeka kwa thamani ya ardhi na vifaa vya ujenzi, jambo linalowafanya wengi washindwe kumudu.
Mtaalam wa kujitegemea wa mipango miji na makazi, Rachel Essau amesema bei ya ardhi na nyumba imepanda katika maeneo mengi nchini na hivyo wanaoweza kumudu ni wachache hasa wenye vipato vikubwa.
“Gharama za maisha ziko juu, mtu anaona badala ya kwenda kununua ardhi ni heri pesa anayopata atumie kujikimu yeye na familia yake hasa kusomesha watoto na matibabu,” amesema Essau.
Mtaalam huyo ambaye anafanyia shughuli zake jijini Dar es Salaam amesema wakati mwingine elimu inachangia ambapo baadhi ya watu wamekosa hamasa ya kumiliki rasilmali hizo na kuwakosesha fursa muhimu ikiwemo mikopo ya benki.
Amesema kuna umuhimu wa Serikali kutoa bei elekezi ya ardhi na nyumba hasa kwa kampuni binafsi zinazotoa huduma hiyo, jambo litakalowasaidia wananchi kujipanga kununua rasilimali hizo.
Soma zaidi:
- Hapa ndipo Watanzania hupatia zaidi kipato chao
- Jinsi ya kufanya mitandao ya kijamii isikuharibie mahusiano yako
- CHATI YA SIKU: Serikali hutumia zaidi mapato katika masuala gani?
Kwa mujibu wa ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ya mwaka 2016 kuhusu mikopo ya ujenzi wa nyumba inaeleza kuwa mahitaji ya nyumba nchini yanakadiriwa kufikia nyumba 200,000 kila mwaka ambapo mpaka sasa kuna upungufu wa nyumba 3 milioni za makazi ya watu hasa katika majiji makubwa kama Dar es Salaam.
Mahitaji ya nyumba yanachochewa zaidi na ongezeko la idadi ya watu kila mwaka na wengine huishia kukaa kwenye nyumba za kupanga au kukodi mashamba kwa ajili kuendesha kilimo.
Wakati matamanio makubwa ya watu yako kwenye nyumba na ardhi, watu wengi wanaweza kununua simu kwa ajili ya mawasiliano hata kama hawana uwezo wa kifedha.
Ripoti ya utafiti huo ambayo ilifanywa na Taasisi ya ukuzaji sekta ya fedha Tanzania (FSDT) kwa ushirika na BoT, Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Zanzibar imesema ni asilimia moja tu ya watu ambao wanatamani kumiliki simu lakini hawawezi.
Hiyo ni sawa kusema mtu mmoja kati ya watu 100 ambaye anatamani kuwa na simu lakini mfuko hamruhudu kuingia kwenye ulimwengu huo wa mawasiliano.