Staa wa Hollywood, Idris Elba na mkewe Sabrina wazuru hifadhi ya Taifa ya Serengeti
- Ujio wa wawili hao umegundulika baada ya Sabrina kuweka picha katika ukurasa wa Instagram ikimuonyesha akiwa na wafanyakazi wa mfuko wa uhifadhi wanyama pori wa Grumeti katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
- Wawili hao wamefika Tanzania mwezi mmoja baada ya kufunga ndoa nchini Morocco.
- Elba ni muigizaji na mwanamziki wa Uingereza wakati Sabrina ni mwanamitindo kutoka Canada.
Dar es Salaam. Kwa mara nyingine tena, Tanzania imepokea ugeni wa staa wa kimataifa wa Hollywood, Idris Elba ambaye yuko nchini kwa matembezi binafsi pamoja na mke wake Sabrina Dhower.
Taarifa za wa wawili hao kuonekana Tanzania zimejulikana baada ya Sabrina kuweka picha katika ukurasa wake wa Instagram akiwa na wafanyakazi wa mfuko wa Uhifadhi wanyama pori wa Grumeti katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Sabrina (29) ameandika katika ukurasa wake wenye takriban wafuasi 273,200, kuwa anawashukuru wafanyakazi wa mfuko huo kwa elimu waliyowapia kuhusu kazi wanazofanya za kuhifadhi mazingira katika hifadhi ya Serengeti.
Huenda safari ya wanandoa hao nchini, ni muendelezo wa mapumziko ya “honeymoon” baada ya kufunga ndoa Aprili 26, 2019 katika hoteli maarufu ya Ksar Char Bagh huko Marrakesh nchini Morocco .
Elba ni muigizaji , mtarishaji, MC na mwanamuziki wa Uingereza mwenye umri wa miaka 46 ambaye amecheza filamu nyingi ikiwemo inayoelezea maisha ya Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela inayoitwa ‘Mandela: WALK TO FREEDOM’
Wakati mke wake Sabrina ni Mwanamitindo aliyezaliwa Marekani lakini ameishi zaidi Canada ambapo alikuwa Mlimbwende wa jiji la Vancouver nchini mwaka 2014 (Miss Vancouver in 2014).
Soma zaidi: Mastaa walivyoitangaza Tanzania kimataifa mwaka 2018
Mastaa wengine ambao wamewahi kutembelea Tanzania na kuipaisha kimataifa katika sekta ya utalii ni pamoja na Rais wa zamani wa Marekani, Barack Obama, mjukuu wa Malkia Elizabeth II wa Uingereza, Prince William na Muigizaji wa filamu muda mrefu kutoka nchini India, Juhi Chawla.
Staa mwingine ni Jodi Sta.Maria kutoka Ufilipino ambaye anafahamika zaidi kwa jina la Maya kutokana na tamthilia maarufu ya ‘Be Careful with My Heart’ aliyoigiza kama msichana wa kazi na kumpa umaarufu duniani.