Serikali yakanusha madai ya Rio kusafisha taswira ya Tanzania kisiasa
- Ufuatiliaji wa Nukta Fakti umebainisha kuwa chapisho linalosambaa halijachapishwa na Habari Maelezo na halipo kwenye kurasa rasmi za mitandao ya kijamii ya chombo hicho cha habari.
Dar es Salaam. Hivi karibuni kuna chapisho ambalo limesambaa kwenye mitandao ya kijamii likidai kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amesema amemleta nahodha wa zamani wa klabu ya Manchester United, Rio Ferdinand kwa lengo la kusafisha taswira ya Tanzania baada ya matukio ya vurugu za Oktoba 29.

Chapisho hilo limechapishwa Mei 22, 2026 kupitia mtandao wa instagram na ukurasa unaojulikana kwa jina la thedartimes likiwa na mfanano wa machapisho ya chombo cha habari cha Serikali cha Habari Maelezo.
“Mauaji yaliyotokea Oktoba 29 yameiachia doa kubwa sana nchi yetu kimataifa. Rio Ferdinand amekubali kutusaidia kuitangaza Tanzania tena duniani ili Nchi yetu iwe safi na watalii waje kwa wingi zaidi. Tukitaka uchumi wetu uendelee kuwa juu, tunawahitaji watu kama Rio Ferdinand” linasomeka chapisho hilo.
Ukweli ni huu
Uchunguzi wa Nukta Fakti imejirishisha kuwa chapisho hilo si halisi na maneno yaliyoandikwa kwenye chapisho hilo hayajasemwa na Waziri Makonda.

Ufuatiliaji wa Nukta Fakti umebainisha kuwa chapisho linalosambaa halijachapishwa na Habari Maelezo na halipo kwenye kurasa rasmi za mitandao ya kijamii ya chombo hicho cha habari.
Aidha, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amethibitisha jana Mei 22, 2026 kwa kuchapisha kwenye mitandao yake ya kijamii kuwa chapisho hilo si halali na ujumbe uliobebwa kwenye chapisho hilo haujasemwa na Makonda.