Serikali kuweka mazingira rafiki mbio za marathon Tanzania
Naibu Waziri wa MaliasiLi na Utalii, Marry Masanja akizungumza na watoto wenye ulemavu walioshiriki mbio za marathon za kilomita tano. Picha |Mariam John.
- Itaandaa vijana wenye vipaji watakaoshiriki mashindano ya kimataifa.
- itazitumia mbio hizo kutangaza vivutio vya utalii.
Mwanza. Serikali imesema itaendelea kuweka mazingira rafiki katika michezo yote hususani riadha ili kuandaa vijana wengi wenye vipaji watakaoshiriki mashindano hayo na kutangaza vivutio vya utalii kimataifa.
Naibu Waziri wa Utalii, Marry Masanja, akizungumza katika kilele cha mbio za Rock City Marathon ambazo zimefanyika jijini Mwanza Oktoba 24 na kushirikisha zaidi ya wakimbiaji 1,000, amesema pamoja na mbio hizo kuimarisha afya ya mwili lakini pia zinasaidia katika kuhamasisha utalii.
“Michezo ni fursa na fursa lazima tuitumie kuandaa vijana watakaowakilisha Taifa kwenye mashindano ya kimataifa, lakini pia itahamasisha kutangaza utalii, na kama serikali tutahakikisha tunaweka nguvu kwenye msimu ujao ili uwe wa kipekee,” amesema Masanja.
Katika mbio za kilomita 5, 10 na 21, Naibu Waziri huyo alitoa ofa kwa washindi kuanzia wa kwanza hadi tatu wa mbio zote kwenda kutalii kwenye kisiwa cha Saanane.
Wakati mashindano hayo yakikikamilika, Mtanzania Alphonce Simbu alishinda mbio za kilomita 21 kwa wanaume huku kwa upande wa wanawake mbio za urefu huo zilichukuliwa na Cheruta Ester kutoka Kenya.
Emmanuel Mzava ni meneja wa benki ya biashara ya Kenya (KCB) mkoani Mwanza anasema wameamua kudhamini mbio hizo ili kukuza ajira.
“Tunaunga mkono Serikali katika suala la ajira , unapotoa ajira kwa vijana unatoa suluhisho kwenye jamii, na sisi kama KCB tumeona ipo haja kudhamini mashindano hayo ili washindi wanapopata zawadi wanakuwa wamewasaidia kwa namna moja ama nyingine kwenye suala la ajira,” amesema Mzava.
Meneja huyo wa tawi la KCB Nyanza amesema katika mashindano hayo walikuwa wamedhamini zaidi ya wakimbiaji 500 waliokimbia mbio za kilomita 10.
Waliangalia kundi hili kwa kwa sababu ni kundi la kati na linaweza kukimbiwa na watu wengi wakiwemo vijana na watu wenye familia.
Anasema huu ni msimu wao wa pili kudhamini mbiyo hizo na kuwa matarajio yao ni kuja kuwa wadhamini wa kuu.
“Riadha inasaidia kutangaza utalii, hivyo tumeona ipo haja ya kusaidiana na Serikali katika kuwasaidia vijana na wafanyabaishara katika kukuza uchumi wa nchi,” amesema Mzava.
Rais wa chama cha riadha nchini, Silas Lukas amesema mbio hizi ni za 22 toka zianzishwe na kuwa kadiri miaka inavyoenda ndivyo zinazidi kukua na kuimarisha uchumi wa nchi.
Anasema washiriki wanatoka maeneo tofauti ndani na nje ya nchi na kuwa baada ya mbio hizo baadhi ya washiriki hutembelea hifadhi za Taifa za Rubondo, Saanane na Burigi Chato.
“Hata sasa ninazo taarifa za washiriki ambao baada ya mbio hizi wataenda kutembelea mbuga ya wanyama Burigi Chato,” amesema Lukas.