Rais Samia ataja mikakati kukabiliana na tembo wavamizi Ruvuma

September 26, 2024 7:42 pm · Yuster Massawe
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni pamoja na kuongeza askari wa wanyama pori na matumizi ya ndege nyuki.
  • Awataka viongozi kutowakatisha tamaa wakulima kutokana na uvamizi wa tembo.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema Serikali yake inatekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kuongeza askari wa wanyama pori na kuongeza doria za wanyama ili kukabiliana na uvamizi wa tembo katika mashamba ya wakulima mkoani Ruvuma.

Rais Samia aliyekuwa akizungumza kwenye mkutano wa hadhara wilayani Tunduru mkoani Ruvuma leo Septemba 26, 2024 amesema Serikali yake inatambua uwepo wa changamoto hiyo na tayari imeanza kuchukua hatua kukabiliana nayo.

“Serikali tumeanza kuchukua hatua, kwanza tumeongeza askari ambao wapo katika maeneo mbalimbali pia kuna askari wa kijiji wanaosaidiana na askari hawa kuhakikisha tembo hawaingii kwenye maeneo ya vijiji, tuna magari ya doria yapo katika wilaya hizi, yanafanya kazi hii,” amesema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia amesema kuwa wameanza matumizi ya ndege nyuki ‘drones’ zinazosaidia kuondoa makundi ya tembo kwenye maeneo ya watu ambapo Rais Samia amesema wataongeza idadi ya drones na kujenga vituo vipya vya askari wa wanyamapori.

Kauli ya Rais Samia inakuja mara baada ya wabunge wa mkoa huo kuiomba Serikali iongeze nguvu kukabiliana na ndovu hao ambao mara kwa mara  wamekuwa wakisababisha uharibifu wa mazao, kujeruhi au kusababisha vifo kwa wakazi wa maeneo hayo jambo linalorudisha nyuma kasi ya maendeleo.

Kwa mujibu wa Mbunge wa Namtumbo Victor Kawawa wastani wa kaya 400 zimeathiriwa na tembo wanaohisiwa kutoka hifadhi ya Mwalimu Nyerere zamani Selou katika vijiji vya Rikuyu na Mandela ambao walilipwa fidia.

Aidha, Wizara ya Maliasili na Utalii nchini Tanzania iliahidi kufanya mashauriano na Wizara ya Fedha ili kukubaliana kifuta jasho kipya kwa watu wanaopata athari za wanyamapori wakali na waharibifu baada ya malalamiko ya muda mrefu ya wananchi na wabunge kuwa viwango hivyo vilikuwa vidogo.

Baadhi ya wabunge waliopigia chapuo mabadiliko hayo akiwemo Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema) Naghenjwa Kaboyoka, aliyesema viwango vya sasa vinamfukarisha mkulima kwa kuwa ekari moja ya mpunga ambayo angeweza kuzalisha magunia 30 yenye thamani ya Sh3 milioni inalipwa Sh100,000.

Kwa mujibu wa Wizara ya Maliasili na Utalii mpaka mwaka 2023 Tanzania ilikuwa na jumla ya tembo 60,000 ikiwa ya tatu nyuma ya Botswana na Zimbabwe.

Hata hivyo, Rais Samia amewataka viongozi kutowavunja moyo wananchi kutokana na uvamizi wa tembo unaoendelea bali waendelee kuzalisha mazao kwa wingi kwa kuwa tayari Serikali yake inafanyia kazi changamoto hiyo huku ikiendelea kutafuta fursa za mazao yanayozalishwa.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...