Mo Dewji: Nilianzisha programu ya wajasiriamali haikufanikiwa
- Hajasema sababu za kushindwa kuendelea kwa programu hiyo.
- Amesema anatafuta mshirika watakayesaidiana kuendesha programu hiyo tena.
- Awataka vijana kufanya kazi kwa bidii kutimiza malengo yao.
Dar es Salaam. Bilionea na mfanyabiashara maarufu wa Tanzania, Mohammed Dewji amesema licha ya programu ya kuwasaidia wajariamali aliyoianzisha kutofanikiwa, amewashauri vijana kufanya kazi kwa bidii huku wakisimamia malengo yao mpaka watakapopata mafanikio wanayokusudia.
“Nilianzisha programu ya Mo Entrepreneurs lakini haikufanikiwa kusema kweli,” amesema Dewji wakati akijibu swali (#AskMoDewji) la mmoja wa wafuasi wake wa Twitter anayejulikana kwa jina la Nelly Msechu (@NellyB52).
Msechu alitaka kufahamu mfanyabiashara huyo anafanya nini kuwasaidia vijana wenye mawazo mazuri ya ujasiriamali lakini hawana mitaji.
Hata hivyo, Dewji ambaye ni mmiliki wa kampuni ya Mohammed Entreprises (MeTL Group) amesema anaangalia namna ya kupata mshirika atakayeshirikiana naye kuendesha programu hiyo ili kuwafaidisha vijana walioingia kwenye ujasiriamali.
“Nia yangu ni kuendelea lakini nahitaji mshirika kusimamia zoezi hilo kusajili na kuwajengea uwezo washiriki, Pamoja na @DewjiFoundation watasimamia, ili biashara hizi zifanikiwe,” amesema Dewji
Zinazohusiana:
- Vijana wazidi kutawala soko la mitandao ya kijamii Tanzania
- Karatasi zisizotumika ofisini ni ‘dili’ kwa vijana
Awataka vijana kusimamia malengo yao
Mafanyabiashara huyo amewashauri vijana waache kujilinganisha na mafanikio ya watu wengine, bali wasimame katika malengo yao waliyojiwekea ili waweze kufanikiwa kimaisha.
“Vitu vingi katika maisha vinaweza kukuzuia usitimize malengo yako lakini usipoteze dira. Mipango inaweza kubadilika lakini siyo hatma yako,” amesema Dewji jana Juni 23, 2020.
Pia amewashauri vijana kuelekeza nguvu zao katika kazi na kuachana na fikra za kupata mafanikio kwa mteremko (shortcuts) kwa sababu hawatayapata.
Latest
