Mmiliki mgodi wa dhahabu matatani uchafunzi wa mazingira
- Ni mmiliki wa mgodi uliopo katika Kijiji cha Maseida mkoani Manyara.
- Anatuhumiwa kuchafua mazingira.
- Kupewa hati ya makosa na kutakiwa kujirekebisha.
Mwanza. Baada ya Mbuge wa jimbo la Mbulu Vijiji Fratel Masei kumlalamikia mwekezaji katika Kijiji cha Maseida mkoani Manyara kusababisha uharibifu wa mazingira, Serikali imetoa agizo la mwekezaji huyo kupewa hati ya makosa ya uchimbaji madini.
Naibu Waziri wa Madini, Dk Steven Kiruswa ametoa agizo hilo baada ya kutembelea eneo hilo la mgodi wa dhahabu amemuagiza Afisa Madini Mkoa wa Manyara, Ernest Sanka kutoa hati ya makosa kwa mwekezaji huyo na asipojirekebisha ndani ya siku 30 afutiwe leseni yake.
Madai ya Mbunge Masei yanahusu kero zinazosababishwa na mwekezaji wa mgodi huo, Paniel Edward ambaye hafuati Sheria ya Madini ikiwemo kutochangia huduma kwa jamii zinazozunguka eneo la mgodi.
“Ninaagiza mwekezaji huyo apewe hati ya makosa ambayo itamtaka kutoa utetezi wake ndani ya siku 30 na akishindwa kufanya hivyo atafutiwa leseni yake,” amesema Dk Kiruswa.
Mwekezaji huyo aliingia mkataba na Serikali ya kijiji kuchangia Sh20 milioni kama mchango wake kwa jamii ambapo mpaka sasa ni zaidi ya mwaka hajatekeleza ahadi yake.
Kamishna wa Madini Dk Abdulrahiman Mwanga amesema Sheria ya Madini inamtaka kila mmiliki wa leseni awe na kibali cha utunzaji wa mazingira ikiwemo kutunza vyanzo vya maji ambayo hutumiwa katika shughuli za nyumbani, kilimo na mifugo.
Amesema wachimbaji wengi wadogo huchafua mazingira kwa kiasi kikubwa kutokana na matumizi ya zebaki kuliko mchimbaji anaetumia teknolojia ya juu katika uchenjuaji.
Dk Mwanga amewataka wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu wanaochimba ndani ya mto kuhakikisha wanakuwa na kibali cha mazingira na kuchenjua madini yao umbali wa mita 60 kutoka mtoni.