Majaliwa ashtukia ajira za “kindugu” stendi ya mabasi Singida
- Amwagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Bravo Lyapembile awaondoe kazini watumishi watatu wanaokusanya mapato kwenye stendi ya mabasi.
- Asema wameajiriwa kindugu huku wakiwa na tuhuma za kuiba mapato.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amemwagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Bravo Lyapembile awaondoe kazini watumishi watatu wanaokusanya mapato kwenye stendi ya mabasi ambao wameajiriwa kindugu huku wakiwa na tuhuma za kuiba mapato.
Majaliwa amesema kuna mchezo unachezwa wa kukusanya mapato lakini hayapelekwi benki na wahusika wakuu ni ni mweka hazina wa Manispaa, Aminieli Kamunde na Mkaguzi wa Ndani, Ibrahim Makana.
“Kuna vijana watatu pale stendi ambao mmewaweka kindugu. Yupo Kennedy Francis (mtoto wa Mkurugenzi); Selemani Msuwa (ndugu yake diwani) na Salehe Rajab Kundya (shemeji yake diwani mwingine). Andika barua leo hii, hawa vijana waondoke kwenye hiyo kazi, na upeleke timu nyingine ya watu waaminifu,” amesema Majaliwa leo (Oktoba 7, 2019) akiwa mkoani Singida.
Amesisitiza wanaohusika kukusanya mapato wahakikishe kila wanapokamilisha makusanyo, wanazipeleka fedha hizo benki na kupatiwa risiti huku akiwasihi Meya na Mwenyekiti wa Halmashauri kutokuingia kwenye mkumbo huo.
“Kuna wakusanyaji wanaoshirikiana na baadhi ya Wakurugenzi na Waweka Hazina. Waheshimiwa Madiwani hakikisheni mnasimamia hizo mashine zinazokusanya mapato na mjue ni nani amepatiwa. Ombeni taarifa mjue nani anayo na yuko wapi,” amesema Majaliwa.
Katika mkutano huo, amehimiza matumizi ya benki na risiti pale pesa zinapohusika ili kuepusha matumizi mabaya ya fedha za umma ikiwa ni lengo la kuhakikisha kuwa fedha zote zinatumika kwa maslahi ya wananchi na siyo vinginevyo.
Zinazohusiana
- Majaliwa awabana watendaji Singida matumizi mabaya fedha za umma.
- Majaliwa atoa neno korosho kukosa wanunuzi.
- Majaliwa awakomalia viongozi Morogoro, amsimamisha kazi mtendaji mwingine.
Pia, Majaliwa amewataka watendaji na mamlaka zote kutumia fedha zinazotolewa na Serikali katika miradi husika na siyo vinginevyo.
“Fedha inayotoka Serikali Kuu ikiletwa inakuja na maelekezo mahsusi. Unakuta fedha inakuja kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya, wao wanahmisha na kujilipa posho au inahamishiwa kwenye mradi mwingine,” amesema Majaliwa.
Majaliwa ameenda mbele zaidi na kumwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Singida, Rashid Mandoa kukamilisha malipo ya madiwani ambayo ni malimbikizo.
Pia amemtaka awasilishe kwenye mfuko wa Hifadhi ya jamii, michango ya madereva ya Sh15,000 ambayo wamekuwa wakikatwa tangu mwaka 2015/2016 lakini haijawasilishwa.
“Hawa walikuwa LAPF, wamekatwa hela zao lakini bado hazijapelekwa.
“Watu hao pia wamekuwa wakikatwa Sh5,500 za bima ya afya tangu wakati huo lakini hadi sasa michango yao haijawasilishwa na matokeo yake wakienda hospitali hawatibiwi. Hakikisha malipo yao yanaenda,” amesema.
Latest