Kila baada ya wiki mbili, lugha moja ya asili inapotea duniani

August 10, 2019 7:55 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Umoja wa Mataifa (UN) umesema  hatua za haraka zinapaswa  kuchukuliwa kuzitunza lugha hizo zilizojaa utajiri wa utamaduni na ufahamu wa maisha.
  • Takribani nusu ya lugha 6,700, idadi kubwa ikiwa ni zile za asili ziko hatarini kutoweka.
  • Elimu, usawa ndiyo njia sahihi za kuhifadhi lugha na jamii ya watu wa asili.

Dar es Salaam. Umoja wa Mataifa (UN) umesema kila baada ya wiki mbili, lugha moja ya asili inapotea duniani huku wito ukitolewa kwa hatua zaidi kuchukuliwa kuzitunza lugha hizo zilizojaa utajiri wa utamaduni na ufahamu wa maisha. 

Miongoni mwa lugha za asili ambazo zimefanikiwa kuhifadhiwa kwa muda mrefu ni lugha ya Kimasai ambayo watumiaji watumiaji wake wanapatikana zaidi katika nchi za Afrika Mashariki. 

Katika taarifa yake ya kuadhimisha Siku ya Kimataifa  ya watu wa asili jana (Agosti 9, 2019), Katibu Mkuu wa UN, Antonio Guterres amesema lugha ni jinsi ambavyo watu wanawasiliana ambapo  ina uhusiano na tamaduni, historia na utambulisho jamii husika. 

Licha ya umuhimu huo, takribani nusu ya lugha 6,700, idadi kubwa ikiwa ni zile za asili, ziko hatarini kutoweka ambapo kila baada ya wiki mbili lugha hutoweka duniani. 

Guterres amesema kwa kila lugha inayotoweka, dunia inapoteza utajiri wa tamaduni na ufahamu unaotokana na watu milioni 370 wanaotoka katika jamii za watu wa asili. 

“Idadi kubwa wanakosa haki zao za msingi, huku mifumo iliyowekwa ya kibaguzi na uenguaji ikiendelea kutishia mbinu zao za maisha, tamaduni  na utambulisho wao,” amesema Guterres.

Katibu Mkuu huyo amesema hali hiyo ni kinyume kabisa na azimio la Umoja wa Mataifa la haki za watu wa asili pamoja na ajenda 2030 ya maendeleo endelevu ambayo inatoa ahadi ya kutomwacha nyuma mtu yeyote.

Amesema ni matumaini  yake kuwa nchi wanachama wa UN zitashirikiana kikamilifu kuhakikisha watu wa asili wanashikiri katika kupanga maendeleo yao kupitia sera shirikishi, za usawa na zinazotekelezeka.


Soma zaidi: 


Siku ya kimataifa ya watu wa asili inayoazimishwa Agosti 9 ya kila mwaka imeenda sambamba na mwaka 2019 ambao ni mwaka wa kimataifa wa lugha za asili ikilenga kusaka hatua za haraka kulinda, kuchagiza na kuendeleza lugha za asili. 

Naibu Katibu Mkuu wa UN, Amina Mohammed amesema jumuiya za kimataifa zinapaswa kuweka mikakati thabiti ya kulinda lugha za asili kwa kutoa elimu sahihi kwa watu wa asili ili wafurahie uwepo wao duniani. 

“Elimu itakuwa na dhima kuu ya kuhakikisha kuwa watu wa asili wanaweza kufurahia na kutunza tamaduni na utambulisho wao. Kushindwa kuweka mfumo wa elimu wenye matumizi ya lugha tofauti na tamaduni za muingiliano kutaweka hatarini watu wa jamii za asili na kutishia uwepo wao,” amesema Mohammed katika taarifa hiyo

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW