Hatari inayowakabili watumiaji wa mshumaa kwa muda mrefu
- Matumizi ya mshumaa katika mazingira yenye mzunguko mdogo wa hewa yanaweza kusababisha maumivu ya kichwa, athari katika mfumo wa upumuaji na homoni.
Dar es salaam. Kwa miongo mingi mishumaa imekuwa ikitumika kama chanzo cha nishati katika baadhi ya nyumba nchini Tanzania na maeneo mengine duniani hususani wakati ambapo matumizi ya umeme hayakuwa yameshika kasi.
Wakati huo, mshumaa ulisaidia kufukuza giza usiku haswa wakati wa mapishi, kula, kufanya usafi na hata wakati wa kujisomea kwa baadhi ya wanafunzi.
Tangu kuanza kwa matumizi yake zaidi ya miaka 5,000 iliyopita, kumekuwa na bunifu mbalimbali zilizobadili matumizi ya mishumaa kutoka kuwa chanzo cha mwanga pekee hadi kuwa mapambo, manukato na wakati mwingine kuwa sehemu muhimu katika baadhi ya madhehebu.
Wakati aina hizo za mishumaa zikishamiri, Shirika la Afya Duniani (WHO) limeonya kuhusu matumizi ya muda mrefu ya bidhaa hizo, kwa sababu huzalisha kemikali kama ‘formaldehyde’ inayoweza kusababisha magonjwa au hata vifo.
Watoto huathirika zaidi
Dk Lameck Christian kutoka hospitali ya Myeku, iliyopo Sumbawanga amesema watoto ndio wanaoathirika zadi na moshi wa mshumaa pamoja na aina nyingine za moshi wa majumbani kwa sababu viungo vyao havijakomaa.
“Mara nyingi watoto ndio huathrika kutokana na kuwa viungo vyao ikiwemo macho na hata mapafu yanakua hayajakomaa, sasa anapokutana na moshi huu inakuwa ni rahisi kupata madhara mengi” amesema Lameck.
WHO inafafanua kuwa magonjwa hayo yatokanayo na moshi wa mishumaa pamoja na moshi mwingine ikiwemo unaotokana na nishati chafu za kupikia huchangia vifo vya watoto 309,000 walio chini ya umri wa miaka mitano na watu wazima milioni 3.2 kila mwaka.

Mishumaa huathiri mfumo wa upumuaji
Moshi unaotokana na mshumaa unaweza kutoa chembechembe ndogo zinazoweza kuingia ndani kabisa ya mapafu, hivyo kwa watu wenye pumu, mzio au magonjwa sugu kwenye mfumo wa upumuaji wanaweza kupatwa na madhara zaidi ikiwemo kukohoa sana, kifua kubana na hata kushindwa kupumua.
Kutokana na hali hiyo, Dk Lameck Christian anashauri wenye magonjwa ya mfumo wa upumuaji, ikiwemo ugonjwa sugu wa kuziba kwa njia za hewa (COPD), kuzingatia ubora wa hewa ndani ya nyumba zao.
“Hakuna hatari ya haraka kwa watumiaji wa mishumaa, lakini kitu cha msingi ni kuwa makini na ubora wa mshumaa unaotumia na kuhakikisha unautumia katika eneo lenye uingizaji mzuri wa hewa” amesema.
Husababisha muwasho wa macho
Mbali na magonjwa katika mfumo wa hewa, Utafiti uliochapishwa katika jarida la Regulatory Toxicology and Pharmacology mwaka 2021 ulibaini kuwa baadhi ya mishumaa huzalisha kemikali na chembechembe ndogo zinazoweza kusababisha muwasho wa macho.
“Baadhi ya mishumaa inapowaka hutoa kemikali na chembechembe mbalimbali hewani, ikiwemo ‘formaldehyde’, ‘benzene’, PM2.5, na oksidi za nitrojeni (NOx ambazo huathiri macho pale mtu anapovuta moshi huo kwa muda mrefu au katika chumba kisicho na hewa ya kutosha,” imesema ripoti hiyo.
Athari katika mfumo wa homoni
Baadhi ya mishumaa yenye manukato imeonekana kuwa na kemikali kama ‘phthalate’, ambazo watafiti wanasema zinauwezo mkubwa wa kuingilia mfumo wa mwili wa homoni na kupelekea mabadiliko yasiyotarajiwa katika mfumo huo.
Daktari na mtaalamu wa tezi na homoni, kutoka Hospitali ya CARE Hill iliyopo nchini India anaeleza kuwa mishumaa inachangia kwa kiasi kikubwa mabadiliko katika mfumo wa homoni.
“Moja ya kemikali za phthalate inajulikana kuharibu homoni, ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa ya kiafya kama vile kupungua kwa uzazi na hata kupelekea mtu kupata saratani” alisema Dk kandula.

Husababisha maumivu ya kichwa
Matumizi ya muda mrefu za gesi hiyo yanaweza kusababisha matatizo ya ubongo, kuathiri uwezo wa mtu kuzungumza na pamoja na kupoteza kumbukumbu.
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Idara ya Mazingira na Nishati nchini Australia, unaeleza kuwa mshumaa huzalisha gesi aina ya ‘Toluene’ ambayo husababisha maumivu ya kichwa, kuchoka na kukosa usingizi, kizunguzungu, kuchanganyikiwa, kusinzia, kupungua kwa umakini na uwezo wa kufikiri.
Mbali na madhara ya kiafya mishumaa pia inaendelea kuwa chanzo cha ajali za moto majumbani pindi inapoachwa ikiwaka bila uangalizi maalumu suala linalohatarisha maisha pamoja na upotevu wa mali.