Google kutoa Sh15.1 bilioni kwa wathibitishaji habari za Corona
- Fedha hizo zitatumika kuzisaidia taasisi na mashirika yanayopambana na habari za uzushi kuhusu Corona.
- Kazi kubwa ya fedha itakuwa ni kuwajengea uwezo waandishi wa habari na kuboresha mifumo ya ufikishaji habari kwa wananchi.
Dar es Salaam. Ili kuhakikisha vita ya kupambana na ugonjwa wa virusi vya Corona (#COVID-19) inafanikiwa duniani, upatikanaji wa taarifa za uhakika na sahihi ni muhimu kwa sababu watu wanataka kufahamu jinsi ugonjwa unavyoambukiza na wanavyoweza kujikinga ili wawe salama.
Wakati watu wakitafuta taarifa sahihi kuhusu COVID-19, baadhi ya watu wenye nia ovu wanatumia mpenyo huo kupotosha kwa kutengeneza habari za uzushi ili kuongeza taharuki na madhara zaidi kwa watu.
Hata hivyo, wadau na mashirika ya kimataifa yamesimama pamoja kuhakikisha yanapambana na taarifa za uzushi ili kuwalinda watu dhidi ya janga hilo la dunia.
Kampuni ya teknolojia ya Google imetangaza kutoa ufadhili wa dola za Marekani 6.5 milioni kwa ajili ya kuzisaidia taasisi na mashirika ya uthibitishaji habari (Fact-checkers) ili kupambana habari za uongo kuhusu ugonjwa wa virusi vya Corona.
Taarifa ya kampuni hiyo ya Marekani iliyotolewa Aprili 2, 2020 inaeleza kuwa mamlaka za afya zimeonya kuwa taarifa nyingi hasa zinazotolewa mtandaoni zinaweza kuwakanganya watu kupata miongozo sahihi kuhusu ugonjwa huo.
“Kuisaidia dunia kutakuwa na maana hasa kama suala la upatikanaji wa taarifa utaangaliwa kwa mapana kwa kuhusisha sayansi, wanahabari, viongozi, majukwaa ya teknolojia na mengine mengi,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Ufadhili huo wa Sh15.1 bilioni utagawanywa kwa mashirika mbalimbali ukiwemo Mtandao wa Kimataifa wa Kuthibitisha habari (IFCN), Chama cha Sayansi cha Marekani (AAAS) na taasisi ya First Draft, ambayo inatoa mafunzo kwa wanahabari wanaoripoti COVID-19 duniani.
Soma zaidi:
Kazi kubwa ya fedha hizo itakuwa kuongeza uwezo wa wathibitishaji habari, kupaza sauti za mamlaka halali za afya, kuboresha mifumo ya ufikishaji habari ambayo inatakiwa kuwasaidia watu kujua nini cha kufanya ili kupunguza athari za COVID-19.
Hata hivyo, Google imesema itaendelea kutumia programu zake ikiwemo Google Trends kufuatilia mwenendo wa ugonjwa huo na kutoa matokeo halisi kwa watu kulingana na maeneo waliyopo.
Nalo shirika lisilo kuwa la kiserikali la Internews limetangaza kutoa ufadhili wa dola za Marekani 100,000 (Sh 231.1 milioni) kuzisaidia kampuni ndogo za habari na za ndani ya nchi duniani kote kuendelea kutekeleza majukumu yake kipindi hiki cha mlipuko wa COVID-19.
Fedha hizo pia zitawasaidia waandishi wa habari kuripoti kwa usahihi habari zinazohusu Corona na kuchangia katika kutokomeza ugonjwa huo.
Latest
