Bila kuchelewesha: Magufuli awateua vigogo wa juu Airtel Tanzania
Dk Omari Nundu aliyeteuliwa na Rais John Magufuli kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Airtel Tanzania. Picha|Mtandao.
- Ni Mwenyekiti na wajumbe wawili wa bodi ya wakurugenzi wa kampuni hiyo.
- Mohammed Mtonga awa mwenyekiti mpya wa bodi ya TTCL kumrithi Dk Omari Nundu anayeenda bodi ya Airtel Tanzania.
Dar es Salaam. Siku moja baada ya Bharti Airtel kuanza kutekeleza sehemu ya makubaliano yaliyofikiwa na Serikali juu ya umiliki wa kampuni ya huduma za simu za mkononi ya Airtel Tanzania, Rais John Magufuli amewateua vigogo wanne kushika nafasi za juu za bodi na menejimenti katika kampuni hiyo ya tatu kwa ukubwa nchini.
Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu iliyotolewa leo (Juni 12, 2019) inaeleza kuwa Rais Magufuli amemteua Dk Omari Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Airtel Tanzania pamoja na wajumbe wawili wa bodi hiyo ambao ni John Sausi na Lekinyi Mollel.
“Uteuzi wa Dk Omari Rashid Nundu katika nafasi hiyo unatokana na makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na kampuni ya Bharti Airtel International juu ya uendeshaji wa kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania ambapo mwenyekiti wa bodi anapaswa kuteuliwa na Serikali ya Tanzania,” inaeleza taarifa kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa.
Kabla ya uteuzi huo, Dk Nundu alikuwa ni Mwenyekiti wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) na ndiye aliyekuwa miongoni mwa vinara walioeleza namna udanganyifu ulivyofanyika kuipunja Serikali katika mchakato wa ubinafsishaji wa kampuni hiyo ya Airtel.
Ili kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Dk Nundu TTCL, Rais Magufuli amemteua Mohammed Mtonga kuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa shirika hilo lililokuwa na asilimia mbili ya wateja milioni 43.62 wa huduma za simu nchini hadi Desemba 2018.
Mtonga ni Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali katika Wizara ya Fedha na Mipango.
Nachukua fursa hii kumpongeza na kumkaribisha mwenyekiti wetu mpya wa bodi ya wakurugenzi @TTCLCorporation Mohammed Abdallah Mtonga na kumpongeza na kumtakia Kila la kheri mwenyekiti wetu Dkt Omari Rashid Nundu kwenye uwenyekiti wake mpya wa bodi ya Airtel. #Tanzania. pic.twitter.com/6lz6vtQKPJ
— WAZIRI KINDAMBA (@wazirik) June 12, 2019
Soma zaidi:
- Waziri Kabudi aeleza ‘walivyotoana jasho’ na kampuni ya Bharti Airtel kupata Sh1 bilioni kila mwezi
- Hisa za Serikali kampuni ya Airtel Tanzania zaongezeka
Mbali na kuwateua mwenyekiti na wajumbe wa bodi wa Airtel Tanzania, Msigwa amesema Rais Magufuli kamteua Dk Prosper Mafole kuwa Ofisa Mkuu wa Ufundi (CTO) wa Airtel Tanzania ikiwa ni sehemu pia ya kutekeleza makubaliano na Bharti Airtel.
Bharti Airtel waliingia katika mgogoro na Serikali baada ya kubainika kuwa mchakato wa ubinafsishaji wa Airtel Tanzania hapo awali uligubikwa na udanganyifu jambo lililomfanya Rais Magufuli kutangaza mwaka 2017 kuwa kampuni ilikuwa ni mali halali ya TTCL.
Hata hivyo, baada ya majadiliano ya awamu tano kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Profesa Palamagamba Kabudi, Serikali ilifikia makubaliano na kampuni ya Bharti Airtel yakiwemo kutoa malipo maalum ya Sh1 bilioni kila mwezi kwa miaka mitano, kubadili muundo wa bodi na menejimenti na kuongeza umiliki wa Serikali kutoka asilimia 40 hadi 49 bila malipo yeyote.
Katika hafla ya makabidhiano ya Sh3 bilioni za malipo maalum ya miezi mitatu ya awali kuanzia Aprili 2019, Mwenyekiti Mtendaji wa Bharti Airtel alieleza kuwa makubaliano hayo ni ya kihistoria na kwamba katika nafasi saba za bodi ya wakurugenzi wa Airtel.