Baada ya Kenyatta, Rais Museveni kutoa Chato kesho
- Atawasili nchini kwa ziara binafsi kama ilivyokuwa kwa Rais wa Kenya.
- Anatarajiwa kukutana na kufanya mazungumzo na Rais John Magufuli kijijini kwake Malimani, Chato.
- Hiyo ni ziara ya pili ya viongozi wa juu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Dar es Salaam. Rais wa Uganda, Yoweri Museveni anatarajia kufanya ziara binafsi ya siku moja nchini Tanzania ambayo itamkutanisha na mwenyeji wake Rais John Magufuli katika Wilaya ya Chato mkoa wa Geita.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa, Museveni atawasili kesho Julai 13, 2019 kwa ajili ya ziara hiyo.
Akiwa hapa nchini, Rais Museveni atamtembelea mwenyeji wake Rais Magufuli nyumbani kwake katika kijiji cha Mlimani kilichopo Wilaya ya Chato.
“Akiwa Chato Mhe. Rais Museveni atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Magufuli,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.
Zinazohusiana: Rais Kenyatta kuzuru Chato kwa mwaliko wa Magufuli
Ziara hiyo ya Rais Museveni inakuwa ni ziara ya pili ya viongozi wa juu wa Jumuiya Afrika Mashariki kutembelea Tanzania ndani ya siku nane.
Julai 5, 2019, Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta alifanya ziara binafsi ya siku mbili katika Wilaya ya Chato ambako alikutana na kufanya mazungumzo na Rais Magufuli.
Akiwa Chato, Rais Kenyatta alikemea baadhi ya tabia za wanasiasa wa Afrika Mashariki kutoa kauli za chuki zinazolenga kujenga uhasama na uadui baina ya wananchi wa jumuiya hiyo.
Baada ya mazungumzo na mwenyeji wake, Rais huyo alikabidhiwa zawadi ya ndege wanne aina ya tausi, ikiwa ni ishara ya uhusiano mwema uliopo kati ya Tanzania na Kenya.