Zifahamu dhana potovu za ulaji wa vyakula kwa mama mjamzito
- Ni pamoja na ulaji wa mayai, samaki na limao.
Dar es Salaam. Katika kipindi cha ujauzito lishe ni miongoni mwa mahitaji ya msingi ikihakikisha upatikanaji wa virutubisho muhimu kwa mama na mtoto aliye tumboni.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) lishe bora inahusisha mlo kutoka makundi yote ya chakula ikiwemo, protini, vitamini na madini ya kutosha.
Baadhi ya makundi hayo yanaweza kupatikana kupitia ulaji wa vyakula mbalimbali kama mboga za kijani na za rangi ya machungwa, nyama, samaki, maharage, karanga, bidhaa za maziwa pamoja na matunda.
Pamoja na kuimarisha afya ya mama vyakula hivyo husaidia katika ukuaji wa ubongo, mifupa na mfumo wa kinga wa mtoto aliye tumboni.
Licha ya umuhimu wa lishe katika kipindi hicho baadhi ya jamii nchini Tanzania zimekuwa zikiwazuia wajawazito kula baadhi ya vyakula kwa madai ya kumduhuru mtoto aliyetumboni suala ambalo halina ushahidi wa kisayansi.
Utafiti uliochaposhwa katika tovuti ya ya PLOS Global Health umevitaja baadhi ya vyakula ambavyo jamii imekuwa ikiwakataza wajawazito, wanawake wanaonyesha na wasichana balehe kula ikiwemo mayai.
Utafiti huo uliofanywa na wanazuoni sita katika mikoa ya Arusha, Mbeya, Singida na Mwanza, umebaini uwepo wa miiko hiyo kwa wajawazito kula ikidai kuwa kufanya hivyo kutamsababishia mjamzito kujifungua mtoto asiye na nywele, mwenye kichwa kikubwa au asiye na afya.
Mwanamvua Zuberi Afisa Lishe kutoka mkoa wa Dar es Salaam, ameiambia Nukta Habari kuwa katazo hilo la mjamzito kula mayai ni mitazamo ya zamani iliyojengwa na mila na tamaduni za baadhi ya jamii.
“Hakuna kundi la chakula ambalo mwanamke anazuIliwa kula ila ni mitazamo ya watu waliojijengea kutoka zamani…mimi niseme ni mila ambazo zimepitwa na wakati,” amesema Zuberi.
Aidha, amesisitiza kuwa mayai ni chakula muhimu kwa mama mjamzito kwa sababu yana virutubisho aina ya protini vinavyohitajika kwa ukuaji na maendeleo ya mtoto tumboni pamoja na vitamini mbalimbali, ikiwemo vitamini A, ambayo husaidia kuimarisha kinga ya mwili wa mama wakati wa ujauzito.
Kwa mujibu wa tovuti ya Apollo Hospital kumzuia mama mjamzito kula mayai kunaweza kusababisha upungufu wa virutubisho muhimu.

Ulaji wa samaki
Katika baadhi ya maeneo nchini Tanzania kuna imani kuwa kula samaki aina ya fulani za samaki husababisha mtoto kuzaliwa na ulemavu suala ambalo halina ushahidi wa kutosha wa kisayansi.
Kulingana na miongozo ya lishe, ikiwemo ile inayosimamiwa na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC), ulaji wa samaki ni muhimu sana kwa mama mjamzito kwa afya yake na ya mtoto aliyepo tumboni kutokan ana wingi wa virutubisho ikiwemo vya Omega-3 (DHA na EPA) ambavyo ni muhimu kwa maendeleo ya ubongo na uwezo wa utambuzi wa mtoto.
Hata hivyo, wataalamu wa afya wanaonya ulaji ya baadhi ya samaki ikiwemo papa kutokana na wingi wa madini ya zebaki (mercury) kwasababu wanaweza kuathiri mfumo wa fahamu wa mtoto.

Ulaji wa pilipili, limao na vyakula vyenye tindikali
Kuna dhana kuwa pilipili au baadhi ya matunda machachu (Citrus fruits) ikiwemo ndimu, limao au mananasi unaweza kusababisha mtoto kuzaliwa na macho mekundu au mabaka mwilini suala ambalo si kweli.
Sharifa Chande mtaalamu wa afya ya binadamu kutoka mkoani Morogoro anaeleza kuwa, mama mjamzito anaweza kula pilipili au limao kwa kiasi cha kawaida kama hana matatizo ya vidonda vya tumbo au kiungulia.
“Ni kweli kwamba vyakula vyenye tindikali vinaweza kuongeza kiungulia au kuwasha tumbo kwa mwenye tatizo hilo (vidonda vya tumbo), lakini kama mama hana changamoto hizo, hakuna sababu ya kuviepuka,” anasema Sharifa.
Tovuti ya Medical news today inabainisha kuwa, limao linaweza hata kusaidia kupunguza kichefuchefu kwa baadhi ya wajawazito ingawa matumizi ya ya limao kupita kiasii yanaweza kuleta usumbufu wa tumbo.
Kula chakula kidogo
Katika baadhi ya jamii, wajawazito hukatazwa kula milo mikubwa kwa hofu ya kupata mtoto mkubwa atakayehitaji upasuaji wakati wa kujifungua.
Imani hii ni hatari kwa sababu inaweza kusababisha mama kupata lishe duni. Mama mjamzito anahitaji kula mlo kamili wenye makundi yote ya chakula kwa kiwango kinachofaa.
Kunyimwa chakula cha kutosha kunaweza kusababisha utapiamlo na kuathiri afya ya mama na mtoto.

Vyakula gani viepukwe?
Kwa upande wa Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) wajawazito wanapaswa kuepuka vyakula vibichi kama maziwa yasiyochemshwa au yasiyopitia usindikaji salama, pamoja na jibini laini iliyotengenezwa kwa maziwa yasiyochemshwa, kwa sababu vinaweza kuwa na bakteria hatari kama Listeria.
Kwa wajawazito wenye kisukari cha mimba (Gestational Diabetes), wanashauriwa kuepuka sukari za viwandani na kula vyakula visivyokobolewa ili kudhibiti kiwango cha sukari mwilini.
Latest