Ujumbe wa kibiashara kutoka Austria kuwasili nchini Januari, 2019

November 16, 2018 11:44 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Utajumuisha makampuni 8 ambayo yanajishughulisha masuala ya afya, usafirishaji na nishati kwa ajili ya kukutana na viongozi na watendaji wa Serikali.
  • Austria imekuwa ikiunga mkono uendelezaji wa miradi ya umeme nchini na hadi sasa wameshatoa mikopo ya masharti nafuu kwa baadhi ya miradi ya umeme iliyo nje ya gridi ya Taifa.
  • Tanzania itapata fursa ya kueleza maeneo yanayohitaji uwekezaji ili kufaidika na ujumbe huo.

Dar es Salaam. Ujumbe wa kibiashara wa makampuni nane kutoka Austria unaotarajiwa kuwasili nchini Januari, 2019 ili kukutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Serikali juu ya fursa za uwekezaji zilizopo nchini. 

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Nishati, ujumbe huo utajumuisha makampuni 8 ambayo yanajishughulisha na masuala ya afya, usafirishaji na nishati na utawasili jijini Dodoma mwishoni mwa mwezi Januari ambapo utasaidia kuimarisha mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na Austria, nchi mwanachama wa Umoja wa Ulaya. 

Katika kuweka sawa maandalizi ya ugeni huo, Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amefanya mazungumzo na Mwakilishi kutoka Ubalozi wa Austria wenye ofisi zake Jijini Nairobi, Kenya, Kurt Mullauer aliyefika wizarani  Dodoma ili kumweleza kuhusu Ujumbe huo wa kibiashara.   

Mullauer amemweleza Naibu Waziri kuwa ujumbe huo wa kibishara unakusudia kuonana na watendaji wa Serikali ili kuangalia namna ya kushirikiana katika maeneo mbalimbali ya biashara na uzalishaji ikiwemo sekta ya umeme ambayo ni muhimu katika ujenzi wa viwanda nchini.  

Ameongeza kuwa, nchi ya Austria imekuwa ikiunga mkono uendelezaji wa miradi ya umeme nchini na hadi sasa wameshatoa mikopo ya masharti nafuu kwa baadhi ya miradi ya umeme iliyo nje ya gridi ya Taifa.


Zinazohusina: Kiswahili ndiyo mpango mzima kusaka wateja Tanzania: Ripoti


Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, aliushukuru ubalozi wa Austria kwa uamuzi waliouchukua wa kuyaleta makampuni hayo nchini ambapo Tanzania itapata fursa ya kueleza maeneo yanayohitaji uwekezaji hasa katika miradi ya uzalishaji umeme ili kuweza kufikia lengo la kuwa na megawati 5,000 ifikapo mwaka 2020.

Naibu Waziri pia amemweleza Mullauer kuwa maeneo ambayo ni muhimu yapewe kipaumbele katika ushirikiano na wawekezaji ni pamoja uzalishaji umeme kwa kutumia maji, gesi asilia na nishati jadidifu na usambazaji umeme vijijini.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amefanya mazungumzo na Mwakilishi kutoka Ubalozi wa Austria wenye ofisi zake zilizopo Jijini Nairobi, Kenya, Kurt Mullauer aliyefika wizarani Jijini Dodoma. Picha| Wizara ya Nishati.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga na Mwakilishi wa Kaimu Kamishna wa Petroli na Gesi, Ebenezer Mollel.

Austria ni nchi isiyokuwa na bandari, imepakana na Ujerumani, Jamhuri ya Czech, Hungary, Slovakia, Slovenia, Italia, Uswisi na Liechtenstein katika bara la Ulaya.

Wakazi wa taifa hilo wapatao milioni 8.5 wanatumia Kijerumani kama lugha yao rasmi.  Ni mwanachama wa Shirika la Kujihami la NATO, pamoja na Umoja wa Ulaya. Mji mkuu wa nchi hiyo ni Vienna na una wakaazi wengi zaidi kuliko miji mengine ya nchi hiyo ambao wanafikia watu milioni 1.8. 

Austria inapakana na safu za milima Alps, ikiwa imegawanyika katika mikoa tisa tofauti.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW