Serikali ilivyojipanga kuinua uchumi wa kidijitali kwa anuani za makazi

October 15, 2021 1:03 pm · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Itatumia zaidi ya Sh45 bilioni kusimika miundmbinu hiyo nchi nzima.
  • Lengo ni kurahisisha ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.
  • Ujenzi wa miundombinu kutoa ajira kwa vijana.

Mwanza. Serikali ya Tanzania inakusudia kutumia zaidi ya Sh45 bilioni kusimika miundombinu ya anwani za makazi, mbawa, nguzo na vibao vya namba za nyumba katika halmashauri 194 ya Tanzania.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk Ashatu Kijaji amesema lengo ni kila mtaa uwe na jina na kila nyumba iwe na namba yake, jambo litakalorahisisha ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

“Uchumi wa kidigitali hauwezi kufikiwa iwapo hatujakamilisha kuweka anwani hizi za makazi,  dhamira ni moja tu kila mtaa na nyumba zitambulike na wizara  yangu tunazo fedha za kutosha na tunaenda kutekeleza hili bila wasiwasi,” amesema Dk Kijaji.

Waziri Ashati amesema mfumo huu wa makazi utapunguza gharama lakini pia kuondoa usumbufu. ikiwemo majanga ya moto.

“Mfano umepatwa na majanga kama, janga la moto, huduma za mizigo na kifurushi zitakufikia kirahisi tofauti na siku za nyuma ambapo hadi utoe maelekezo ambayo yalikuwa yanapoteza muda,” amesema waziri huyo kuwa fedha hizo ziko katika bajeti ya mwaka 2021/22.

Hadoi sasa, jumla ya halmashauri 21 nchini zimefikiwa na huduma ya anuani ya makazi, jambo linalorahisisha ifikishaji wa vifurushi katika maeneo ya kazi, ofisi na biashara.

Katibu Mkuu wizara hiyo, Dk Zainab Chaula amesema  awali utekelezaji wa mfumo huu ulifanyika nchi nzima lakini haukuwa na mafanikio na kuwa walichagua Jiji la Mwanza kama jiji la mfano.

Amesema zaidi ya  Sh1.6 bilioni zimetumika kusimika miundombinu yote ya anwani za makazi, mbawa, nguzo na vibao vya namba za nyumba katika mitaa yote 175 ya jiji la Mwanza.

“Jiji la Mwanza lilionyesha kufanya vizuri kati ya halmashauri zote nchini, tukaona ipo haja ya kuweka nguvu kwenye halmashauri hiyo ili zingine zije zijifunze, viongozi na watendaji katika mitaa wametoa ushirikiano na wamefanya vizuri,” amesema Dk Chaula.

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew (kushoto) akionyesha vibao vinavyoonesha majina ya barabara katika Manispaa ya Musoma hivi karibuni ikiwa ni moja ya miundombinu ya mfumo wa anwani za makazi na postikodi unaotekelezwa chini ya wizara hiyo kwa ushirikiano na Ofisi ya Rais Tamisemi na Wizara vya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Picha| Mtaa kwa Mtaa.

Fursa kwa vijana

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel amesema atakutana na vijana na vikundi ambavyo vinaweza kutengeneza vibao vya nyumba ili kuchangamkia fursa hiyo.

Amesema kwa sasa nguzo na vibao hivyo vinatengenezwa Jijini Dar es Salaam pekee  na kusafirishwa kwenda mikoani kitendo ambacho hutumia gharama kubwa tofauti na vingetengezwa kwenye mkoa husika.

“Mfumo huu unaenda kuleta mapinduzi makubwa na kwamba kama Serikali tutahakikisha zoezi linafikiwa kirahisi, hivyo niwaombe vijana wajitokeze kuchangamkia fursa hiyo,” amesema mhandisi Gabriel.

Mwenyekiti wa kamati ya wataalam wa anwani  za makazi na postikodi, Masese Seleki amesema mpaka sasa jumla ya nguzo 5,823 zimewekwa kwenye mitaa jijini hapa.

Aidha jumla ya vibao vya nyumba 106,824 vimetolewa na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya habari ambapo hadi sasa jumla ya vibao vya nyumba 78,138 zimetumika kuweka kwenye nyumba zilizopo jijini hapa.

“Hadi sasa nyumba 98,000 zimeingizwa kwenye mfumo  wa anwani  za makazi na postikodi, zoezi ambalo limeonyesha mafanikio makubwa ,” amesema Seleki.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW