Rais Samia aunda tume kuchunguza usawa wa kijinsia Tanzania

September 22, 2021 5:54 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link

Rais Samia akiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Biashara Duniani (WTO), Ngozi Okonjo Iweala kwenye mazungumzo nchini Marekani. Picha| Ikulu Tanzania.


  • Itaangalia namna bora ya Tanzania kupata usawa wa kijinsia.
  • Pia inapitia marekebisho ya sheria, na sera kandamizi kwa wanawake.
  • Amesema usawa wa kijinsia utasaidia kuondoa umaskini kwa wanawake.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameunda timu ya wataalamu ambao wanaangalia namna bora ya Tanzania kupata usawa wa kijinsia wakati wa uongozi wake ili kutokomeza umaskini miongoni mwa wanawake.

Timu hiyo inatarajiwa kuja na mapendekezo kadhaa ya kuwainua wanawake kiuchumi na kijamii ili kuhakikisha kundi hilo linapata fursa mbalimbali na kuondokana na umasikini unaowakabiri.

Timu hiyo kwa sasa inapitia marekebisho ya sheria kandamizi, sera na mikakati ya kuwasaidia wanawake katika kupata fursa katika nyanja mbalimbali ikiwemo ajira, elimu, umiliki wa ardhi, kupata mikopo na nafasi za uongozi.

Licha ya kuunda tume hiyo, tayari Rais Samia ameanza kuchukua hatua mbalimbali kuongeza fursa za usawa wa kijinsia hasa katika vyombo vya maamuzi katika Serikali yake.

“Hivi karibuni nimemteua Waziri wa Ulinzi (Dk Stergomena Tax) ambaye amekuwa mwanamke wa kwanza kushikilia nafasi hiyo nchini mwetu, ili kuondokana na dhana kuwa wanawake wanaweza nafasi fulani tu,” amesema Rais Samia Septemba 21, 2021 katika mkutano maalum wa wakuu wa nchi na wanawake uliofanyika Jijini New York, Marekani.

Amesema uteuzi huo wa wanawake  utaondoa dhana ya kuwa kuna nafasi ambazo wanawake hawawezi kuzishika.

Rais Samia pia ametoa wito kwa washiriki wenzake katika kikao hicho kutokutoa fursa kwa Uviko-19 kuwa kikwazo cha kuzuia mafanikio katika usawa wa kijinsia na kusisitiza kuwa ili Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (SDG’s) kufanikiwa, lengo namba 5 kuhusu usawa wa kijinsia ni lazima lipewe kipaumbele.

Pamoja na hayo, Mkuu huyo wa nchi amekutana na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Biashara Duniani (WTO), Ngozi Okonjo Iweala aliyezungumza naye kuhusu kuwezesha biashara kwa kuimarisha upatikanaji wa chanjo, usimamizi wa uvuvi na kilimo.

Enable Notifications OK No thanks